DIWANI APIGA MARUFUKU MIKOPO MITAANI KUEPUSHA BALAA



DIWANI wa Ndembezi, Manispaa ya Shinyanga, David Nkulila ambaye pia ni Mwenyekiti wa Mtaa wa Mabambasi, amepiga marufuku baadhi ya watu kukopeshana fedha kienyeji huku wakidai riba kubwa ndani ya mwezi mmoja hali inayoleta migogoro ndani ya jamii.

Diwani huyo amesema kuna watu kwenye kata hiyo wanaokopesha wenzao wanaohitaji fedha kwa haraka na kuwatoza riba.

Amesema biashara hiyo inaikosesha Serikali mapato.

Nkulila amesema hivi sasa amepiga marufuku ukopeshwaji wa namna hiyo, kwanza wanakwepa kulipa mapato ya serikali kwani wamekuwa wakienda kwenye ofisi za serikali za mitaa kwa ajili ya kuandikishana ukopaji huo.

Amesema kuwa wapo baadhi ya watu wamekuwa wakijitokeza kukopesha mfano kiasi cha Sh 150,000 wakitaka kulipwa na aliyemkopesha Sh 300,000 ndani ya mwezi mmoja akishindwa kulipa hapo unatokea mgogoro mkubwa kati yao.

"Nimepiga marufuku ukopeshwaji huo wa kienyeji hata kuwaandikia makubaliano kwenye ofisi ya mtaa tumekataa, uliona wapi riba inakuwa kubwa namna hiyo ndani ya mwezi mmoja, wengi wamekuwa wakishindwa kurejesha fedha hizo matokeo yake kumekuwepo migogoro katika jamii," amesema.

Ofisa Maendeleo ya Jamii, kata ya Ndembezi, Jackson Njau, amesema kata hiyo ina vikundi zaidi ya 100 lakini kati ya hivyo vikundi 75 ni vya wanawake na viko hai na biashara wanayoifanya walio wengi ni mamalishe na wauza mbogamboga.

IMEANDIKWA NA KARENY MASASY- habarileo SHINYANGA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527