MGEJA AUSHTUKIA UBUNGE WA MAMA SALMA KIKWETE ALIOPEWA NA RAIS MAGUFULI


ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja amemuomba Mke wa Rais Mstaafu, Mama Salma Kikwete kuutafakari kwa makini uteuzi wa ubunge alioteuliwa Machi 1,2017 na Rais John Magufuli.

Mgeja ambaye pia ni Mwenyekiti wa taasisi inayoshughulika na utawala bora ya Tanzania Mzalendo Foundation, amesema nafasi aliyofikia mama Salma akiwa mke wa rais mstaafu na ‘First Lady’ wa nchi ni nafasi kubwa kiitifaki hivyo anapaswa kuwa na heshima na abakie kuwa mama mshauri na mlezi wa taifa.

“Namuomba Mama Kikwete aige mfano wa mama Regina Lowassa (mke wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa) ambaye wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu mwaka 2015 na baada ya uchaguzi Chadema ilimpa heshima kwa kumteua kuwa Mbunge wa Viti Maalumu lakini kwa heshima aliikataa nafasi hiyo.

“Mke wa rais mstaafu siyo mtu au kiongozi mdogo lazima tujiulize inapotokea akachangia hoja ndani ya bunge ikapingwa au aambiwe kaa chini au toka nje au atolewe nje na askari wa bunge je, hiyo heshima au aibu na fedheha inaenda kwa nani?” amehoji Mgeja.

Pamoja na mambo mengine, Mgeja amesema wake wa viongozi ni sehemu ya viongozi ambapo ana mashaka itifaki ndani bungeni inaweza kugongana hivyo amemtaka Mama Salma Kikwete akapokea ushauri na mitazamo ya watu mbalimbali na isimaanishe kwamba anamuonea wivu kwani maamuzi yanabaki kwake kukataa ama kukubali ushauri huo kama changamoto katika kupanga na kuchagua.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527