Picha:MGODI WA ACACIA BULYANHULU WALIPA ZAIDI YA SHILINGI BILIONI 1 YA USHURU WA HUDUMA HALMASHAURI YA MSALALA NA NYANG'WALE



Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu uliopo katika halmashauri ya Msalala wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga umekabidhi hundi zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya malipo ya ushuru wa huduma kwa halmashauri ya Msalala iliyopo mkoani Shinyanga na halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale mkoani Geita.



Hafla fupi ya kukabidhi hundi hizo imefanyika Alhamis Machi 2,2017,katika ukumbi wa halmashauri ya Msalala wilayani Kahama na kuhudhuriwa na viongozi wa halmashauri na mikoa ya Shinyanga na Geita pamoja na viongozi mbalimbali kutoka mgodi wa Acacia Bulyanhulu. 


Akizungumza wakati wa hafla hiyo,Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew alisema fedha hizo ni malipo ya ushuru wa huduma kwa ajili ya kipindi cha miezi sita kuanzia mwezi Julai hadi Disemba 2016. 

Alisema fedha hizo ni asilimia 0.3 ya ukokotoaji wa ushuru wa huduma ya mgodi huo kwa kipindi cha miezi sita katika awamu ya pili kuanzia mwezi Julai hadi Disemba 2016. 

“Mgodi umelipa shilingi za kitanzania 1,135,178,526/= na malipo hayo yamegawanyika katika halmashauri mbili kwa mujibu wa makubaliano na serikali ambapo halmashauri ya Msalala imelipwa shilingi milioni 760 sawa na asilimia 67 na Nyang’wale shilingi milioni 374 sawa na asilimia 33”,alisema Crew. 

Aidha alisema mpaka sasa mgodi huo umelipa jumla ya shilingi bilioni 4.3 tangu mwaka 2014 kampuni ya Acacia ilipoanza kutoa malipo ya ushuru wa huduma wa asilimia 0.3 ya mapato ghafi kwa halmashauri husika. 

“Katika kipindi cha miaka hiyo minne halmashauri ya Msalala imelipwa zaidi ya shilingi bilioni 3.7 na Nyang’wale imelipwa shilingi bilioni 1.1”,aliongeza Crew. 

Katika hatua nyingine Crew alisema mgodi huo unaendelea kushirikiana na serikali na wadau wa maendeleo ili kutekeleza miradi mbalimbali kwa ajili ya kuboresha huduma endelevu za kijamii na miundombinu katika jamii hususani katika elimu,barabara,umeme,maji na huduma za afya.

Wakipokea hundi hizo,mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga na Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela waliushukuru mgodi huo kwa kutimiza wajibu wa kulipa kodi na kuongeza kuwa fedha hizo zitatumika katika shughuli za maendeleo ya wananchi katika halmashauri za Msalala na Nyang'wale.

Mwandishi mkuu wa Malunde1 blog,Kadama Malunde alikuwepo wakati wa hafla hiyo,ametuletea picha za matukio yaliyojiri,tazama hapa chini 
Wa pili kutoka kulia ni Mtaalamu wa Mawasiliano Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu Mary Lupamba akiwakaribisha viongozi wa mkoa wa Shinyanga na Geita wakati wa hafla fupi ya kukabidhi hundi zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya malipo ya ushuru wa huduma kwa halmashauri ya Msalala na Nyang’wale.Wa kwanza kushoto ni Meneja mkuu wa mgodi wa Bulyanhulu Graham Crew,akifuatiwa na mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga na Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela 
Meneja mkuu wa mgodi wa Bulyanhulu Graham Crew akiangalia hundi ya shilingi milioni 374 kabla ya kuikabidhi kwa mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga kwa ajili ya halmashauri ya wilaya ya Nyang'wale .Kushoto ni Kiongozi wa Kitengo cha Mahusiano ya Jamii mgodi wa Bulyanhulu Sarah Ezra Teri 
Meneja mkuu wa mgodi wa Bulyanhulu Graham Crew akikabidhi hundi yenye thamani ya shilingi milioni 374 kwa mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga kwa ajili ya malipo ya ushuru wa huduma ya mgodi kwa halmashauri ya Nyang'hwale iliyopo mkoani Geita 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akishikana mkono na mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga wakati akikabidhi hundi ya shilingi milioni 374 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akizungumza wakati wa kukabidhi hundi zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja kwa ajili ya malipo ya ushuru wa huduma kwa halmashauri ya Msalala iliyopo mkoani Shinyanga na halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale mkoani Geita. Alisema halmashauri ya Msalala imelipwa shilingi milioni 760, Nyang’wale shilingi milioni 374 
Mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga akikabidhi hundi hiyo ya shilingi milioni 374 kwa mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale Carlos Gwamagobe 
Mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga akizungumza wakati wa zoezi la makabidhiano ya hundi yenye thamani ya shilingi milioni 374 kwa ajili ya halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale ambapo alisema fedha hizo zitatumika katika shughuli za maendeleo ya wananchi katika halmashauri hiyo 
Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale Carlos Gwamagobe (kulia) akishikana mkono na Mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga wakati wa makabidhiano ya hundi hiyo 
Mkuu wa wilaya ya Nyang’wale Hamim Gwiyama akishikana mkono na Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew wakati wa makabidhiano ya hundi ya shilingi milioni 374 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew (kushoto) akizungumza wakati wa kukabidhi hundi yenye thamani ya shilingi milioni 760 kwa ajili ya malipo ya ushuru wa huduma ya mgodi kwa halmashauri ya Msalala iliyopo mkoani Shinyanga. Katikati ni katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela akifuatiwa na mbunge wa jimbo la Msalala Ezekiel 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akishikana mkono na katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela wakati wa kukabidhi hundi ya shilingi milioni 760 kwa ajili ya halmashauri ya wilaya ya Msalala iliyopo wilayani Kahama mkoani Shinyanga 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akizungumza wakati wa kukabidhi hundi hiyo ambapo alisema halmashauri ya Msalala imelipwa shilingi milioni 760 sawa na asilimia 67 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akizungumza wakati wa makabidhiano hayo ya hundi ya shilingi milioni 760 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akishikana mkono na mbunge wa jimbo la Msalala wilayani Kahama Ezekiel Maige 
Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela akizungumza wakati wa kupokea hundi yenye thamani ya shilingi milioni 760 ambapo alisema aliushukuru mgodi huo wa malipo ya ushuru na kuongeza kuwa tayari fedha hizo zimeshaingizwa kwenye bajeti ya halmashauri ya Msalala kwa ajili ya maendeleo ya halmashauri hiyo. 
Meneja mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu Graham Crew akishikana mkono na Mweka hazina  halmashauri ya Msalala Masatu Mnyolo aliyemwakilisha mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala wakati wa kukabidhi hundi hiyo 
Mbunge wa jimbo la Msalala Ezekiel Maige akizungumza wakati wa makabidhiano hayo ambapo aliuomba mgodi huo kuendelea kulipa kodi kama inavyostahili huku akiomba mgodi kuyabana makampuni yanayofanya kazi zake mgodini ili yalipe kodi kwa ajili ya maendeleo ya halmashauri ya Msalala 
Meneja Mkuu wa Mahusiano ya Kampuni ya Uchimbaji ya Acacia na Serikali Mhandisi Asa Mwaipopo akizungumza wakati wa makabidhiano hayo ambapo alisema Acacia imetimiza wajibu wa kulipa ushuru na kufanya tukio la kukabidhi hundi hizo kwa uwazi zaidi ili kuepuka minong'ono kuwa pengine mgodi huwa haulipi kodi 
Meneja Mkuu wa Mahusiano ya Kampuni ya Uchimbaji ya Acacia na Serikali Mhandisi Asa Mwaipopo alisema kodi iliyolipwa imetokana na uzalishaji wa mgodi kwa kipindi cha miezi sita na hiyo ni awamu ya pili,utaratibu wa Acacia ni kulipa kwa miezi 6 na tayari awamu ya kwanza walishalipa na sasa wamemalizia kipindi cha pili katika mwaka 2016 
Meneja Mkuu wa Mahusiano ya Kampuni ya Uchimbaji ya Acacia na Serikali Mhandisi Asa Mwaipopo alisema kampuni ya Acacia imekuwa ikifanya kazi zake kwa kushirikiana na wananchi wanaozunguka migodi yao
Meneja Mkuu wa Mahusiano ya Kampuni ya Uchimbaji ya Acacia na Serikali Mhandisi Asa Mwaipopo akishikana mkono na mbunge wa jimbo la Msalala Ezekiel Maige
Meneja Mkuu wa Mahusiano ya Kampuni ya Uchimbaji ya Acacia na Serikali Mhandisi Asa Mwaipopo akiagana na katibu tawala mkoa wa Shinyanga Albert Msovela.

Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527