RAMAPHOSA KUAPISHWA KUWA RAIS WA AFRIKA KUSINI


Cyril Ramaphosa Mwenyekiti wa chama tawala cha ANC Cyril Ramaphosa anatarajiwa kuapishwa kuwa rais wa Afrika Kusini baada ya rais wa taifa hilo Jacob Zuma kujiuzulu.

Bwana Zuma alikuwa chini ya shinikizo kali kutoka kwa chama chake cha ANC kilichomtaka ajiuzulu la sivyo akabiliwe na kura ya kutokuwa na imani dhidi yake bungeni.

Katika taarifa ya runinga, alisema kuwa anajiuzulu mara moja lakini hakubaliani na uamuzi wa chama.

Bwana Zuma anakabiliwa na madai kadhaa ya ufisadi lakini amekana kufanya makosa yoyote.

Akiwa naibu wa rais Ramaphosa anakuwa kaimu wa rais mara moja baada ya Zuma kujiuzulu.

Taarifa ya serikali inasema kuwa bunge litamchagua rais mpya wa Afrika Kusini Alhamisi jioni.

Bwana Zuma ,mwanachama wa jeshi la ANC wakati wa ubaguzi wa rangi, alipitia nyadhfa kadhaa za chama hicho hadi kuwa rais.
Image captionCyril Ramaphosa na Jacob Zuma

Aliliongoza taifa hilo kwa muda mrefu baada ya ubaguzi wa rangi.

Lakini anaachilia madaraka akikabiliwa na kashfa kadhaa huku uchumi wa Afrika kusini ukiwa katika hali mbaya.

Siku ya Jumatano, maafisa wa polisi walivamia nyumba ya Johanesburg ya familia ya Gupta iliokuwa na ushawishi mkubwa serikalini.

Familia hiyo imeshutumiwa kwa kutumia urafiki wao wa karibu na rais Zuma kujilimbikizia ushawishi mkubwa wa kisiasa .

Hata hivyo familia hiyo imekana hayo.

Nini kinafanyika sasa?

Kwa mujibu wa katiba , iwapo kutatokea pengo katika wadhifa wa rais, aliyeko chini ya wadhifa huo anakaimu urais:

(a) Naibu rais

(b) Waziri aliyechaguliwa na rais

(c) Waziri aliyechaguliwa na mawaziri wengine katika baraza

(d) Spika wa bunge, hadi bunge litakapomchagua mmoja wao kuchukuwa wadhifa huo.

ANC kimeshinda kila uchaguzi Afrika kusini tangu kumalizika kwa utawala wa ubaguzi wa rangi mnamo 1994.

Kama naibu rais, na pia mwenyekiti wa chama tawala ANC. Bwana Ramaphosa ndiye anayepokea wadhifa huo.

Licha ya taarifa za awali kwamba angependa kuchukuwa muda uliosalia kujitayarisha kwa uchaguzi wa mwakani, akiwa ndiye kaimu rais hivi sasa, anatarajiwa kuapishwa rasmi kama rais na bunge.

Nini hatma ya ANC?

Chama cha ANC kimeshinda kila uchaguzi Afrika kusini tangu kumalizika kwa utawala wa ubaguzi wa rangi mnamo 1994.

Kwa raia wengi wa Afrika kusini ndiyo chama kilichowaletea uhuru dhidi ya uovu na utawala uliogubikwa na ubaguzi wa rangi, na hili sio jambo linaloweza kusahaulika kwa urahisi.

Lakini umaarufu wake umekuwa ukififia , na kwa mara ya kwanza kuna uwezekano wa kweli kwamba huenda chama hicho kikapoteza uongozi - hususan iwapo upinzani utaunga muungano.

ANC kilipata pigo la aibu katika uchaguzi wa serikali za kieneo mnamo 2016.

Licha ya kwamba kilipata kura zaidi dhidi ya vyama vingine, kilipoteza miji mikubwa ukiwemo mji mkuu kibiashara wa Johannesburg na Pretoria.

Wakati hapana shaka kwamba maisha ya raia wengi nchini yameimarika, wengi wanahisi yaliobadilika hayajatosha chini ya utawala wa chama hicho cha ANC.
Wajumbe wa ANC huchaguliwa kutoka matawi mbali mbali kote nchini

Afrika kusini bado ni mojawapo wa mataifa yasio na usawa duniani na zaidi ya nusu ya idadi ya watu wanaoishi nchini humo wanaishi katika umaskini.

Tuhuma za rushwa katika serikali ya ANC zimeongeza chumvi kwa hisia iliopo kwamba kundi fulani la matajiri walio na uhusiano na wanasiasa wanafaidi huku raia wa kawaida wakiteseka.

Pia kuna hisia miongoni mwa Waafrika weusi nchini kwamba ngazi ya uongozi iliyoundwa chini ya utawala wa ubaguzi wa rangi bado ikaliko.

Hususan katika masuala ya ardhi na uchumi.

Ugavi mpya wa ardhi iliyonyakuliwa kutoka kwa mtu mweusi wakati wa utawala wa kibepari unachukua muda mrefu mno kutekelezwa.

Takriban 95% ya mali ghafi nchini ipo mikononi mwa asilimia kumi ya raia nchini.

Na Wazungu raia wa nchi hiyo bado wanalipwa mara tano zaidi ya wenzao weusi.

Chama cha ANC kimeahidi kushinikiza ugavi huo wa ardhi - kiasi cha kuahidi kuibadili katiba kuruhusu kuichukuwa ardhi iliyokuwa imenyakulia, bila ya wamiliki wa sasa kulipwa fidia.

Na kimeidhinisha sera ya "mageuzi makali ya kiuchmi" - inayonuia kurudisha uongozi wa kiuchumi mikononi mwa iadi kubwa ya watu weusi nchini.


Lakini iwapo kinataka kuendelea kushikilia sifa na imani ya uwekezaji, tchama hicho pia kinahitaji kuwashawishi wafanya biashara kwamba Afrika kusini haitofuata mkonodo iliyoufuta Zimbabwe.


Kusawazisha maslahi ya wapiga kura dhid ya wafanyabiashara na huenda uchumi ukaishia kuwa changamoto kubwa kwa chama cha ANC huku uchaguzi mkuu ukitarajiwa mwakani 2019.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527