SERIKALI YA TANZANIA KUNUNUA NDEGE NYINGINE MPYA MWEZI JULAI

Serikali iko kwenye mpango wa kuongeza ndege nyingine moja ili zizidi kufika sehemu nyingi zaidi Tanzania ambapo Naibu Waziri wa wizara ya Ujenzi, uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Edwin Ngonyani amesema Julai 2017 ndio inanunuliwa nyingine.


Amesema Ndege hiyo itakayonunuliwa July ni aina ya Dash 8-Q 400 ambapo hatua hiyo italifanya shirika la ATCL kufikisha Ndege nne (4) ambazo zitaongeza safari zake kwa kuhudumia masoko yake ya ndani na miji ya Nchi jirani kama vile Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Malawi, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo(DRC).


Ni kauli ambayo aliitoa wakati wa uzinduzi wa safari za Ndege za ATCL kwenye mkoa Tabora na kuongezea kwamba lengo la Serikali ni kuhakikisha hadi kufikia July 2018 Shirika la Ndege Tanzania liwe linamiliki Ndege sita zenye uwezo wa kubeba abiria kwa kiwango tofauti tofauti na kusafiri mikoa mingi na nje ya Tanzania.


Naibu Waziri alisema hadi sasa Serikali imeshanunua ndege mbili aina ya Bombardier Dash 8-Q400 zenye uwezo wa kubeba abiria 76 kila moja na hatua inayofuata ni ununuzi wa ndege nyingine tatu aina ya Bombardier Dash 8-Q400 yenye uwezo kubeba abiria 76, CS 300 mbili zitakazobeba abiria 132 kila moja na Boeing 787 ya kubeba abiria 262.


Alisema kuwa hatua hiyo inaenda sambamba na uimarishaji wa Shirika la Ndege hapa nchini na ujenzi wa viwanja vipya vya ndege katika mikoa ambayo haina viwanja hivyo kwa sasa ili ifike siku mikoa yote Tanzania iweze kuunganishwa na usafiri wa anga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527