Picha 17: JAMAA ANAYEDAIWA KUWALA URODA WAKE ZA WATU KISHIRIKINA SHINYANGA AKAMATWA,ASHUSHIWA KIPIGO


Mwanamme aliyejitambulisha kwa jina la Shaban Charles(30) amejikuta katika wakati mgumu baada ya kushushiwa kipigo  na wananchi wa kitongoji cha Buyambelele Magharibi kijiji cha Bugayambelele kata ya Kizumbi katika manispaa ya Shinyanga wakimtuhumu  kuwaingilia wanawake nyakati za usiku kisha kufanya nao mapenzi kwa njia za kishirikina.Anaripoti Kadama Malunde



Tukio hilo limetokea leo majira ya saa kumi jioni ambapo wakazi wa kitongoji cha Bugayambelele Magharibi jirani na kijiji cha Nhelegani kilichokumbwa na taharuki ya kuwepo mtu anayefanya mapenzi na wanawake kimazingara.

Wananchi hao walimshtukia jamaa huyo baada ya kuonekana akifanya vitendo walivyodai kuwa vya kishirikina katika familia mbili za kitongoji hicho hali iliyosababisha wamhusishe moja kwa moja na tukio lililozua gumzo katika kata hiyo la mtu asiyejulikana kufanya mapenzi na kuiba mali za wananchi kishirikina.

Wakizungumza na Malunde1 blog wakazi  wa eneo hilo walisema mtu huyo aliingia kwenye nyumba mbili(kaya mbili ya James Shilugu na Masele Shija) bila kupiga hodi huku akidai kuwa alikuwa anatafuta mke wake,akidai kuwa ametoka kwa mganga wa kienyeji kaelekezwa kuwa mke wake yupo eneo hilo amejificha.

Hata hivyo baada ya wananchi kumtilia mashaka, jamaa huyo alianza kukimbia na kutupa simu zaidi ya tatu za mkononi alizokuwa nazo wananchi wakafanikiwa kumkamata wakaanza kumpiga kisha kumpeleka kwenye mkutano wa sungusungu na walipompekua wakamkuta na dawa za kienyeji zinazodaiwa kuwa za mapenzi,zikisomeka kama ifuatavyo;

“Imala yose -kuchoma kuomba mke wako roho yake ili irudi kwako aje kwako”na nyingine maandishi yakisomeka "kuoga na kuchoma kuomba mkeo akupende na arudi kwako”.

Wakazi wa eneo waliendelea kumshambulia mtu huyo kwa kutumia silaha za jadi ikiwemo fimbo na marungu kabla ya askari wa jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga kufika eneo la tukio kisha kumpandisha kwenye gari na kuondoka naye.

Wakazi wa eneo hilo waliofikiwa na mwanamme huyo Masele Shija na Francis Shilugu kutoka familia ya James Shilugu na Masele Shija walisema vitendo alivyokuwa anafanya mwanamme huyo havikuwa vya kawaida.

“ Huyu jamaa alifika hapa akakaa kwenye zizi la ng’ombe,Kulikuwa na mtoto anacheza nje ya nyumba,tukamwambie hebu muangalie huyo mtu anafanya nini hapo,akamuuliza kulikoni uko hapa,jamaa akasema natafuta mke wangu amekuja kutafuta nyumba apange, akamuuliza unasema kweli?,ndipo jamaa akachukua baiskeli yake aliyokuwa ameiweka kwenye minyaa akaichukua na kukimbia ndipo akaibukia kwenye familia ya James Shilugu”,alieleza Masele Shija.

“Alikuwa na baiskeli alipofika karibu na nyumbani kwetu akailaza chini,ghafla nikamuona anaingia ndani baadaye akatoka ndani ya nyumba yetu,nikamuuliza wewe nani na umeingiaje humu tena bila hodi,akasema anatafuta mke wake ameingia ndani na mwanamme na amepotea kimiujiza”,alisema.

“Nikaita majirani,tukampeleka kwenye kengele(mkutano wa sungusungu),walipoanza kumuuliza maswali akaanza kukimbia,wakamkimbiza wakamshika,alikuwa na simu akazitupa akabakiza moja tu”,alieleza Francis Shilugu.

Mmoja wa wakazi wa eneo hilo Suzan Stanslaus alisema kutokana na vitendo alivyokuwa anaonesha mwanamme huyo kulikuwa na dalili za wanawake kuingiliwa kimwili kwa njia za kishirikina usiku kwani wamekuwa wakisikia taarifa za wanawake kubakwa na wanaume kulazwa nje ya nyumba katika kijiji jirani cha Nhelegani.

“Mimi nilikuwa nyumbani kwangu wakaja wanakijiji wakiwa na mwanamme huyu wakidai ndiye amekuwa akiwafanyia mchezo mchafu akina mama usiku na kuiba simu za watu,na leo alipokamatwa alikuwa na simu nyingi na dawa za kienyeji”,alieleza Stanslaus.

Akizungumza kwa tabu na Malunde1 blog ,mwanamme huyo alisema anaitwa  Shaban Charles (30) kutoka kata ya Kitangiri katika manispaa ya Shinyanga na amefika hapo akitokea kwa mganga wa kienyeji kijiji Mwamala kufuata dawa za kutafuta mke wake aliyeachana naye na amegoma kurudi nyumbani.

“Nilikwenda kwa mganga baada ya kuelekezwa kwa mganga huyo akanipa dawa za kuoga na kuchoma akaniambia mke wangu yupo hapa

Mwenyekiti wa kitongoji cha Bugayambelele Magharibi Donald Francis alisema alipigiwa simu na kuelezwa kuwepo kwa mwanamme anayehusishwa na tukio la kubaka wanawake kishirikina na kuiba simu katika kijiji jirani cha Nhelegani kata ya Kizumbi.

Alisema mwanamme huyo alikutwa na dawa za kienyeji huku akitoa maelezo yasiyoeleweka ikiwemo kudai amefika hapo kwa ajili ya kutafuta kazi ya kufyatua matofali,kutafuta mke wake na anatoka kwa mganga wake wa kienyeji aliyemnyweshwa dawa za ajabu.

Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga Elias Mwita alipotafutwa na waandishi wa habari alisema hana muda kuzungumza na waandishi wa habari mpaka baadaye.
Angalia picha hapa chini

Mwanamme aliyejitambulisha kwa jina la Shaban Charles kutoka Kitangiri katika manispaa ya Shinyanga anayedaiwa kujihusisha na vitendo vya kubaka wanawake kishirikina nyakati za usiku-Picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Polisi wakiwa eneo la tukio


Wananchi wakiwa eneo la tukio

Dawa za kienyeji alizokutwa nazo jamaa huyo

Dawa za kienyeji za jamaa pamoja simu yake..dawa imeandikwa
“Imala yose -kuchoma kuomba mke wako roho yake ili irudi kwako aje kwako”

Dawa za kienyeji "kuoga na kuchoma kuomba mkeo akupende na arudi kwako”.

Polisi na wananchi wakiwa wamemzunguka jamaa huyo

Mwandishi wa habari wa Radio Faraja Steve Kanyeph akifanya mahojiano na jamaa huyo

Wananchi wakiwa eneo la tukio

Wananchi wakiwa eneo la tukio

Gari la polisi likiwasili eneo la tukio


Jamaa akipanda kwenye gari la polisi

Baiskeli ya mtuhumiwa ikipandishwa kwenye gari la polisi


Polisi wakiondoka na mtuhumiwa

Wananchi wakiondoka eneo la tukio
Mwenyekiti wa kitongoji cha Bugayambelele Donald Francis akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema alipigiwa simu na kuelezwa kuwepo kwa mwanamme anayehusishwa na tukio la kubaka wanawake kishirikina katika kijiji jirani cha Nhelegani kata ya Kizumbi.
Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog 
SOMA <<HAPA >>HABARI KUHUSU WANAWAKE KUBAKWA KICHAWI SHINYANGA 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527