Na Dotto Kwilasa,Dodoma
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za pole kwa Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azan Zungu, kufuatia kifo cha Mbunge wa Peramiho, Mhe. Jenista Mhagama.
Katika salamu hizo, Rais Samia amesema:
"Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Mbunge wa Peramiho, Mheshimiwa Jenista Mhagama,natoa pole kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azan Zungu; wananchi wa Jimbo la Peramiho; familia, jamaa na marafiki."
Aidha, Rais Samia ameeleza kuwa kwa kipindi cha miaka 38, Mhagama amelitumikia Taifa kwa weledi na uaminifu kama mwanachama mahiri wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kiongozi wa vijana na wanawake, Waziri katika awamu mbalimbali za Serikali, na mshauri wa wengi katika siasa na maisha.
Amehitimisha salamu zake kwa kumwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi.
Taarifa hii imetolewa kupitia akaunti rasmi ya Rais kwenye mtandao wa Instagram.

Social Plugin