Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

WIKI YA HUDUMA KWA MTEJA: NSSF SHINYANGA YAGUSA MAISHA YA WAFUNGWA KWA MSAADA WA KIJAMII


Katika kuelekea maadhimisho ya Wiki ya Huduma kwa Mteja, wafanyakazi wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) mkoa wa Shinyanga wamefanya tukio la kipekee la kutoa huduma kwa jamii, kwa kutembelea Gereza la Wilaya ya Shinyanga na kutoa msaada wa mahitaji mbalimbali kwa wafungwa walioko gerezani.

Katika tukio hilo la kugusa maisha ya wenzetu wanaopitia changamoto, NSSF imetoa msaada wa vitu muhimu zikiwemo sabuni, miswaki, mafuta, nguo, pamoja na vifaa vya kufanyia usafi.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Meneja wa NSSF Mkoa wa Shinyanga, Bi. Amina Mdabi, alisema kuwa lengo la tukio hilo ni kurudisha kwa jamii na kutambua kuwa hata wale walioko magerezani bado ni sehemu ya jamii, na wanapaswa kuonjeshwa upendo na mshikamano wa kijamii.

“Tunajua kuwa wenzetu walioko ndani bado ni sehemu ya jamii yetu. Mwisho wa siku, watarejea uraiani na kuendelea na maisha yao kama kawaida. Tumezungumza nao na kuwaeleza kuwa hata wao wana nafasi ya kujiunga na NSSF, ili waanze kujiwekea akiba kwa ajili ya maisha yao ya sasa na baadaye,” alisema Mdabi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Shinyanga, Bw. Kizito Kunambi, alitoa shukrani kwa NSSF kwa msaada huo, akibainisha kuwa si kila mfungwa anayeingia gerezani ana familia au ndugu wa kumsaidia.

“Tunashukuru sana kwa msaada huu. Serikali peke yake haiwezi kugharamia kila kitu, na ukweli ni kwamba baadhi ya waliopo hapa hawana ndugu kabisa. Msaada huu utasaidia kuleta utulivu, faraja na kuimarisha hali ya kisaikolojia ya wafungwa wetu,” alisema Kunambi.

Tukio hili ni sehemu ya mikakati ya NSSF ya kuimarisha uhusiano na jamii, sambamba na kuhamasisha umuhimu wa hifadhi ya jamii kwa kila Mtanzania – bila kujali hali yake ya sasa. Katika Wiki ya Huduma kwa Mteja, NSSF inaendelea kuonyesha kuwa huduma kwa wateja si tu ofisini, bali ni pia kujali ustawi wa jamii nzima.






Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com