NG'OMBE 12 WAKUTWA WAKICHINJWA NDANI YA LORI

Ngombe 12 wanaosadikiwa kufa jana wamekutwa wakichinjwa ndani ya lori eneo la mtaa wa Wazo jijini Dar es salaam kwa ajili ya kusambazwa kwenye mabucha ya ngo’mbe.

Mmoja wa mashuhuda Issa Ibrahim amesema wakati anaelekea msikitini jana saa 10 alfajiri aliliona gari aina ya lori limesimama pembezoni mwa barabara na alipolisogelea aliwaona watu wakiwachuna ng’ombe waliokufa.

Amesema aliwahoji na kuwakataza wasiendelee kuwachuna ngombe hao kwa kuwa dini hairuhusu kula vibudu lakini watu hao walikaidi na kuendelea kazi yao.

“Wale watu walikuwa wengi kila mmoja alikuwa na kisu chake huku wakichuna ngombe hao, kwa kuhofia usalama wangu nilipiga simu msikitini ndipo walikuja eneo hili ili tuungane tuweze kuwakamata lakini wote walikimbia na kuacha nyama zao kwenye gari,” amesema Ibrahim.

Katibu wa Kamati ya Afya na Mazingira mtaa huo, Ally Kitokos amesema matukio ya kuchinjwa ng’ombe waliokufa hujitokeza mara kwa mara na ndiyo maana hivi karibuni mmiliki wa machinjio ya Wazo alimfukuza kazi mchinjaji mkuu baada ya kupingana na kitendo cha kuchinja ngombe waliokufa.


“Leo hii tunaona ng’ombe 12 wamekufa kibudu na wanaendelea kuwachuna kwa ajili ya kupelekwa kwenye mabucha, wakati mchinjaji mkuu wa mwanzo alifukuzwa kwa kosa hilo,” amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527