MBOWE ASHANGAA SUGU KUTOKA GEREZANI

Kufuatia kuachiwa huru kwa Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi na Katibu wa Chadema Nyanda ya Juu Kusini, Emmanuel Masonga kutoka Gereza la Ruanda, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, amesema bado hawajafahamu ni taratibu gani zimetumika kuwaachia huru wakati kifungo chao kilikuwa bado.


“Katika mazingira ya kawaida, siku yao ya kifungo walichokuwa wamepewa kilikuwa kinaishia Juni 5, mwaka huu, lakini ghafla wakapewa taarifa kwamba wataachiwa leo. Hatuna hakika sana ni taratibu gani zimetumika kufupisha kifungo chao kwa sababu jambo hilo halijawekwa wazi.


“Tangu wamewekwa gerezani ni takribani miezi mitatu, mawakili wetu walifanya jitihada za kuhakikisha rufaa yao katika mazingira ya dharura inasikilizwa, lakini haikuwahi kupata jaji wala kusikilizwa kwa sababu kila jaji aliyepangiwa kesi hiyo alionekana ana udhuru,”alisema Mbowe.


Aidha, amesema wao wanaamini kesi hiyo haikuwa ya haki kwa sababu watuhumiwa walinyimwa dhamana mwanzoni, na kutokana na mazingira ya kesi yenyewe hawakutakiwa kupewa kifungo. 


Pia amedai kwamba wataendelea na rufaa yao ili kuweka rekodi sawa na kudhihirisha kwamba Sugu na Masonga hawakuwa na makosa.


Sugu na Masonga walitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miezi mitano jela Februari 26 mwaka huu katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya kwa kutoa lugha ya fedheha dhidi ya Rais John Magufuli kwenye mkutano wa hadhara walioufanya Desemba 30 mwaka jana eneo la Shule ya Msingi Mwenge jijini Mbeya.


Wawili hao wameshatumikia adhabu hiyo kwa siku 73 ikiwa ni zaidi ya robo ya kifungo chao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527