WAZIRI MKUU AKABIDHI MILIONI 5 KWA MJASIRIAMALI MWENYE ULEMAVU WA MIGUU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemkabidhi Bibi Tecla Hamidu ambaye ni mlemavu wa miguu sh. milioni tano ili aweze kuongezea katika mtaji wake.


Ametoa fedha hizo leo (Jumanne, Machi 20, 2018) ikiwa ni katika kutimiza ahadi yake aliyoitoa Februari 22, 2018 kwenye Mkutano wa Sita wa Wamiliki wa Viwanda na Watumiaji wa simbomilia (barcodes).


Waziri Mkuu alitoa ahadi hiyo baada ya Bibi Tecla ambaye ni mjasiriamali anayejihusisha na ushonaji wa bidhaa mbalimbali zikiwemo nguo kumuomba amchangie sh. 500,000 ili aweze kuongezea mtaji wake.


Wakati akimkabidhi fedha hizo, Waziri Mkuu amesema kwamba anatarajia zitamsaidia katika kuongeza mtaji wake, hivyo atazalisha bidhaa nyingi zenye ubora unaohitajika katika masoko ya ndani na nje.


Kwa upande wake, Bibi Tecla alimshukuru Waziri Mkuu kwa msaada huo na ameahidi kuzitumia fedha hizo kama ilivyo kusudiwa.


“Nashukuru kwa msaada huu kwani kuna watu wanakopa sh. laki mbili ili waongeze mitaji, lakini mimi leo nimepewa milioni tano bure na kiongozi wetu,”


Amesema licha ya kukabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa masoko anaamini tatizo hilo litakuwa historia baada ya kuwa na mtaji wa kutosha kwani atakwenda kuzalisha bidhaa zenye ubora zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527