TRENI YA TANZANIA HADI RWANDA KUTUMIA UMEME


RWANDA na Tanzania zimekubaliana kujenga reli ya kisasa (SGR) ya umeme kutoka Isaka, Kahama mkoani Shinyanga hadi Kigali, Rwanda badala ya ile ya awali iliyokuwa iwe ya kisasa lakini yenye kutumia nishati ya dizeli.

Wataalamu wanasema treni ya umeme ni bora zaidi lakini pia ni rafiki wa mazingira ikilinganishwa na treni inayotumia dizeli. Wakati wa mkutano wao wa pili mjini Kigali, Mawaziri wa usafirishaji wa nchi zote mbili, waliagiza Shirika la Maendeleo ya Usafirishaji la Rwanda (RTDA) na Kamati ya Pamoja ya Ufuatiliaji (JTMC) kupitia upya upembuzi yakinifu kwa niaba ya nchi zote mbili kabla ya kuanzisha Kitengo cha Utekelezaji Mradi (PIU).

Waziri wa Nchi wa Rwanda (Usafirishaji), Jean de Dieu Uwihanganye na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Tanzania, Profesa Makame Mbarawa, mwishoni mwa wiki walisaini tena makubaliano mengine ya utekelezaji wa mradi huo. Muda uliopangwa kuanza kwa ujenzi wa reli hiyo itakayounganisha Bandari ya Dar es Salaam na Kigali, umebaki kuwa Oktoba, 2018.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kusainiwa makubaliano hayo, Uwihanganye alisema mabadiliko hayo yametokana na ukweli “tunataka kupunguza muda na gharama za usafirishaji wa abiria na bidhaa kati ya Dar es Salaam na Kigali na kuiboresha reli hiyo. Hiyo ndiyo sababu ya kupitiwa upya kwa upembuzi yanikifu.” Profesa Mbarawa alisema serikali zote mbili zitapitia upembuzi huo baada ya taratibu za manunuzi na huenda ikawa ndani ya mwezi mmoja.

Katika mpango wa kutumia treni ya umeme, treni ya abiria itakuwa ikisafiri kwa mwendokasi wa Kilometa 160 kwa saa na ile ya mizigo itakuwa ikisafiri kwa mwendokasi wa Kilometa 120 kwa saa,” alisema Profesa Mbarawa. Imeelezwa kuwa umbali kati ya Dar es Salaam na Kigali ni Kilomita 1,320. Hivyo, kwa mabadiliko hayo, inaweza kuchukua saa 15 kwa mzigo kusafirishwa kutoka Dar es Salaam hadi Kigali wakati abiria wakitumia saa 10 kusafiri.

Aidha, reli hiyo ya kisasa kutoka Bandari ya Dar es Salaam hadi Kigali inatarajiwa kugharimu Dola za Marekani zipatazo bilioni 2.5 (Sh trilioni 5.5 za Tanzania). Imeelezwa kuwa Tanzania itachangia dola bilioni 1.3 wakati Rwanda itachangia dola bilioni 1.2. Waziri Mbarawa na ujumbe wake walikuwa nchini Rwanda kwa ziara ya kikazi ya siku mbili na walirudi nchini juzi jioni. Unafuu wa bidhaa Kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya uchumi, reli ya kisasa inayotarajiwa kujengwa na kuziunganisha Tanzania na Rwanda itapunguza sana gharama za usafirishaji mizigo.

Kwa Rwanda inakadiriwa kuwa reli itakapoanza kutumika itapunguza gharama za usafirishaji kwa wastani wa Dola za Marekani 1,500 (Sh milioni 3.3 za Tanzania) kwa kila kontena, hivyo kuleta unafuu wa bidhaa kwa watumiaji. Kwa sasa, Rwanda inakadiriwa kusafirisha tani 950,000 za mizigo kwa mwaka kiasi ambacho kitapaa zaidi reli ya kisasa itakapoanza kazi. Uganda inanufaika pia kwa barabara lakini pia kwa usafiri wa majini kwa kupitishia mizigo yake Ziwa Victoria, Mwanza ambako mizigo hufikishwa kwa treni inayotoka Dar es Salaam.

Wasafirishaji wa mizigo wa Rwanda wanasema kwa wastani, huwagharimu Dola za Marekani 4,990 (Sh milioni 11 za Tanzania) kusafirisha kontena la urefu wa futi 20 wakati katika nchi nyingine na Kusini mwa Jangwa la Sahara, kwa kontena la aina hiyo, gharama yake inakadiriwa kuwa Dola 2,504 (Sh milioni 5.5 za Tanzania). Hata hivyo, Waziri Uwihanganye amesema kwa sasa gharama ya kusafisha kontena moja kati ya Kigali na Dar es Salaam ni wastani wa Dola za Marekani 3,912 (Sh milioni 8.6 za Tanzania).

Alipotakiwa kulinganisha umbali kati ya Dar es Salaam-Kigali upande wa Korido ya Kati na ile ya Korido ya Kaskazini, Mombasa-Kampala-Kigali, Kayitakirwa alisema; “Ya Kaskazini ni ndefu, kilometa 1,661 na ina mipaka miwili ya kuvuka tofauti na Korido ya Kati inayolazimu kupita mpaka mmoja wa Rusumo, tena umbali ni kilometa 1,495 tu.” Kwa mujibu wa Shirika la Taifa la Takwimu la Rwanda, bandari ya Dar es Salaam ndiyo inayotumika kupitisha mizigo mingine ya Rwanda kwa zaidi ya asilimia 80, wakati ile ya Mombasa mizigo ni wastani wa asilimia 20 na 30.

Theodore Murenzi, dereva na mmoja wa wasafirishaji wa mizigo wa Rwanda, anasema malori kati ya 200 na 250 huvuka mpaka wa Rusumo kuingia au kutoka Rwanda na Tanzania kila siku. Tayari Rwanda imeanza kujenga vituo kadhaa vikubwa vya stesheni za reli nje ya Jiji la Kampala. Stesheni kubwa ya abiria inajengwa Ndera, wilayani Gasabo wakati ile ya mizigo inajengwa Masaka, wilayani Kicukiro.

Chanzo- Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527