Breaking : RAIS AJIUZULU..WAZIRI MKUU ATOA TAARIFA



Rais wa Mauritius, Ameenah Gurib-Fakim amelazimika kujiuzulu baada ya kuandamwa na kashfa ya fedha.

Taarifa za kujiuzulu kwake zimetangazwa leo Machi 10, 2018 na Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Pravind Jugnauth.

Gurib-Fakim, ambaye ni rais pekee mwanamke barani Afrika ameshutumiwa kwa kutumia kadi ya benki iliyotolewa na shirika moja lisilo la kiserikali kwa ajili ya matumizi yake binafsi.

Atajiuzulu wadhifa huo Machi 12, 2018 wakati Taifa hilo litakapoadhimisha miaka 50 ya uhuru.

" Rais wa Jamhuri ameniambia kuwa anajiuzulu na tumekubaliana tarehe ya kuondoka,” amesema Jugnauth wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Port Louis.

Katika miezi ya hivi karibuni kumekuwa na mfululizo wa matukio ya marais barani Afrika kuachia madaraka kwa kushurutishwa au kujiuzulu kwa hiari.

Miongoni mwa mataifa yaliyoshuhudiwa hali hiyo ni pamoja na Afrika Kusini, Zimbabwe na Ethiopia.

Rais huyo wa Mauritius aliingia madarakani mwaka 2015 kama rais wa heshima na kuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo katika Taifa hilo.

Amekuwa akiandamwa na shinikizo kali tangu gazeti la L'Express lilipochapisha taarifa zilizoeleza jinsi taasisi moja ya Uingereza ilivyompatia kadi ya benki iliyomwezesha kufanya manunuzi ya hali ya juu katika maduka mbalimbali.

Taasisi hiyo ya Planet Earth Institute imekuwa ikidhaminiwa na bilionea wa Angola ,Alvaro Sobrinho ambaye anachunguzwa kutokana na kashfa mbalimbali ikiwamo utakatishaji wa fedha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527