Breaking : LORI LAUA WATU SABA KIGOMA....TAZAMA LILIVYOSAMBARATIKA VIPANDE VIPANDE

Na Rhoda Ezekiel- Malunde1 blog

Watu saba wamefariki dunia katika ajali ya gari aina ya Scania katika  Mlima wa Kasagamba kijiji cha Mkongoro barabara ya kutoka Manyovu wilaya ya Kigoma Vijijini kuelekea mkoani Kigoma.


Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani Kigoma Maltini Otieno amesema ajali hiyo imetokea leo Machi 21,2018 majira ya saa tatu asubuhi. 

Amesema gari aina ya Scania lori yenye namba T741AAB  ilianguka na kusababisha vifo vya watu saba akiwemo dereva wa gari hiyo aliyefahamika kwa jina la Siri Hamis (43) mwenyeji wa Singida pamoja na utingo wake aliyefahamika kwa jina la Ramadhani Saidi (23) mkazi wa Manyoni.

Kamanda Otieno amesema katika gari hiyo walikuwa wamebeba mizigo na watu wanne mmoja mwanamke na wa tatu wanaume ambapo wote walifariki na majina yao hayakufahamika.

Aidha amesema ajali hiyo pia imesababisha kifo cha mwanafunzi aliyefahamika kwa jina la Eliakimu Samsoni (15 )aliyekuwa akitembea kwa miguu kuelekea shuleni na gari hilo kumgonga akiwa anatembea.


Amesema chanzo cha ajari hiyo ni dereva kushindwa kuimudu gari kwenye mteremko mkali na kusababisha gari hiyo kutelemka kwa mwendo mkali na kumshinda dereva huyo na kusababisha vifo hivyo.

Kamanda Otieno amewaomba madereva kuzingatia sheria za barabarani na kuhakikisha gari za mizigo hazibebi abiria ili kunusuru vifo vitokanavyo na ajali na kuhakikisha wanazingatia alama za barabarani.
Mabaki ya lori baada ya ajali - Picha na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527