SERIKALI KUGHARAMIA MAZISHI YA MWANAFUNZI ALIYEPIGWA RISASI NA POLISI DAR





Serikali imetoa pole kwa familia ya mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwiline aliyeuawa kwa kupigwa risasi Februari 16,2018 na kuahidi kugharamia mazishi yake.



Akizungumza leo Februari 18,2018 na vyombo vya habari, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako amesema pamoja na katibu mkuu wa wizara watahakikisha wanasimamia shughuli zote za msiba huo.


Amesema Akwilina alikuwa katika majukumu yake ya kawaida akipeleka barua yake ya mafunzo kwa vitendo Bagamoyo alipofariki dunia.


"Mafunzo yake kwa vitendo yalikuwa yanatarajiwa kuanza Februari 26, mwaka huu, hivyo kifo chake kimeleta simanzi kwa wananchi wote na Serikali kwa jumla.”


"Akwilina alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi wa kike waliojipambanua kwa kujua umuhimu wa elimu, alihakikisha anasoma kwa bidii kwa manufaa yake na familia yake, lakini pia alinufaika na mkopo wa elimu ya juu," amesema Profesa Ndalichako.


Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Masauni amesema uchunguzi wa tukio hilo utafanyika haraka iwekezanavyo, kwa weledi na utaalamu ili haki itendeke.


"Tutafanya uchunguzi na kuwachukulia hatua kali za kisheria wote watakaobainika kuhusika na tukio hilo, Serikali tunasikitishwa na kifo cha mwanafunzi huyu, pia na kujeruhiwa raia na askari polisi wawili," amesema Masauni.


Amesema Serikali haiwezi kuyaacha matukio hayo yapite kama yalivyo, hivyo imeyachukulia kwa uzito unaostahili.


Chanzo- Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527