MWANAFUNZI WA KIKE KIDATO CHA TANO ANUSURIKA KUFA KWA KUNYWA SODA YENYE SUMU


Mwanafunzi wa kike Glory Mushi (20) anayesoma kidato cha tano katika shule ya sekondari ya Milundikwa wilayani Nkasi katika mkoa wa Rukwa amenusurika kifo baada ya kunywa soda inayosadikiwa kuwa na sumu akidaiwa kutaka kujiua.

Mwanafunzi huyo ambaye amelazwa kwa matibabu katika Hospitali ya Misheni iliyopo katika Kasta ya Chala wilayani Nkasi anaishi katika hosteli shuleni hapo.

Muuguzi Msaidizi aliyekuwa zamu hospitalini hapo , Elizabeth Chele alikiri kumpokea mwanafunzi huyo akiwa mahututi ambapo baada ya vipimo vya kitabibu imebainika kuwa alikunywa kinywaji baridi 'soda' kilichochanganywa na sumu ya kuua panya.

“Baada ya kumpatia matibabu mgonjwa sasa afya yake imeanza kuimarika japo bado hawezi kujieleza vizuri lakini ni imani yetu hayupo tena kwenye hatari ya kifo “, alieleza .

Akizungumzia tukio hilo lililotokea jana mchana Msaidizi wa Mkuu wa Shule ya Sekondari Milundikwa Thomas Mapunda alisema kuwa msichana huyo alirejea shuleni hapo jana mchana akitokea kutibiwa katika hospitali ya Rufaa mkoa wa Rukwa iliyopo mjini Sumbawanga.

Kwa mujibu wa Mwalimu wa Taaluma shuleni hapo Charles Mwamengo alisema kuwa mwanafunzi huyo alikuwa kwenye hosteli ya shule ambapo alikuwa akinywa kinywaji baridi lakini ghafla alianza kupiga kelele akilalamika kuhisi maumivu makali tumboni.

“Ndipo tulimshirikisha Diwani wa Kata hii , Richard Mpemba … tukamkimbiza Hospitali ya Misioni iliyopo katika Kata ya Chala akiwa mahututi kwa matibabu baada ya kupewa huduma ya kwanza wauguzi walisema hawaoni sababu ya kumpeleka katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Nkasi mjini Namanyere kwa matibabu kwa kuwa wanamudu kuokoa maisha yake “ alieleza .

Kwa upande wake Diwani wa Kasta ya Milundikwa Mpemba alisema kuwa hadi sasa bado hajajulikana chanzo cha mwanafunzi huyo kutaka kujiua kwa sababu bado hali yake haijatengemaa sawa sawa.
Na Walter Mguluchuma- Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527