DC SHINYANGA AFUNGUA KIKAO CHA TAHOSA SHINYANGA, ATOA TAHADHARI KWA WAKUU WA SHULE


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akifungua kikao cha Umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSA) halmashauri ya wilaya ya Shinyanga (Vijijini) .Kushoto ni mwenyekiti wa TAHOSA wa halmashauri hiyo Leonard Laurent. Kulia ni Kaimu mkurugezi wa halmashauri hiyo Stewart Makali. picha na Kadama Malunde - Malunde1 blog

 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine MatiroMatiro amewatahadharisha wakuu wa shule za sekondari wilayani humo kutothubutu kuchangisha pesa kwa wazazi na wanafunzi kwa ajili ya mitihani ya shule na shule kwani ni kwenda kinyume cha agizo la rais John Pombe Magufuli linalokataza michango shuleni.


Matiro ametoa tahadhari hiyo leo Jumatano Februari 7,2018katika kikao cha kwanza kwa mwaka 2018 cha Umoja wa wakuu wa shule za sekondari Tanzania (TAHOSA) halmashauri ya wilaya ya Shinyanga (Vijijini) kilichofanyika  katika ukumbi wa Mwalimu House Mjini Shinyanga na kuhudhuriwa na wakuu wa shule 27 za sekondari zilizopo katika halmashauri hiyo. 


Aidha aliwataka wakurugenzi wa halmashauri za wilaya kutumia mapato ya ndani na juhudi za wafadhili au wadau wa elimu kufanikisha mitihani ya wilaya badala ya kuchangisha wazazi na wanafunzi. 

"Naomba mitihani mnayofanya ya Interschool Examination isihusishe michango yoyote kutoka kwa wazazi na wanafunzi, tukihusisha michango tunakuwa tumekwenda kinyume na kanuni, taratibu na matamko yanayotolewa na viongozi wetu”,alisisitiza . 

"Hakikisheni pia pesa za serikali zinatumika kulingana na kanuni na utaratibu uliopangwa,zisipotumika vizuri maana yake mmeshindwa kufanya kazi mtawajibishwa”,alieleza. 

Mkuu huyo wa wilaya aliwakumbusha kuwa wakuu wa shule ndiyo wasimamizi wakuu wa shule na mambo yanapoharibika wao ndiyo watakuwa wa kwanza kuchukuliwa hatua. 

“Kwa mwongozo uliopo sasa mkuu wa shule ndiye mdhibiti ubora wa shule wa kwanza, yaani ubora wa shule unakutegemea wewe, ina maana shule yako ikiwa na matatizo msababishi ni wewe na mwalimu mwandamizi wa taaluma, tumieni vizuri vitabu vya mwongozo mlivyopewa, kiongozi cha mwalimu mkuu ili kujikita katika mazingira salama mnapotekeleza majukumu yenu", alisema Matiro. 

Mkuu huyo wa wilaya pia aliwataka wakuu hao wa shule kusimamia nidhamu kwa walimu na wanafunzi na kudhibiti utoro shuleni. 

Matiro aliwataka walimu kujituma katika kazi na kuzitaka mamlaka zinazohusika kuwachukulia hatua walimu ambao shule zao kila mara zimekuwa zikifanya vibaya katika matokeo ya mitihani. 

“Mwalimu upo pale kila mwaka wanafunzi wanafeli, wanapata ziro, shule inakuwa ya mwisho halafu mnamuacha tu huyo mwalimu kwanini? tuna walimu wengine pelekeni wakajaribu Labda kuna tatizo linalosababisha hayo maana kuna mtu mwingine kapewa majukumu yanayomzidi uwezo, mwekeni pembeni aingie mwingine tuone mabadiliko”,aliongeza. 

Matiro aliwakumbusha pia wakuu wa shule kuwajengea wanafunzi hulka ya kupenda michezo na kuwapatia elimu ya kujitegemea badala ya kuwapa elimu ya darasani pekee na 

Kwa upande wake mwenyekiti wa wakuu wa shule za sekondari halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Leonard Laurent alisema pamoja na nia njema ya rais Magufuli kuzuia michango shuleni,jamii imelipokea agizo hilo tofauti ambapo wazazi na jamii kwa ujumla hawajishughulishi na chochote katika maendeleo ya shule. 

“Jamii sasa haijishughulishi na chochote,hata pale walipokuwa wameshaazimia wao wenyewe kuchangia gharama za samani (viti na meza),chakula na miundo mbinu kupitia kamati walizounda wenyewe hawashiriki tena”,alieleza. 

Aidha aliwaomba viongozi wa serikali kuzunguka kila kata ili kukutana viongozi wa kata na wenyeviti wa serikali za vijiji ili watoe fasiri sahihi juuu ya nafasi ya ushiriki wa jamii katika kuleta maendeleo ya shule zao. 
Imeandikwa na Kadama Malunde - Malunde1 blog

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akifungua kikao cha wakuu wa shule za sekondari katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga leo Jumatano. Aliwasisitiza kutumia pesa  zinazotolewa na serikali kama inavyotakiwa.
Wakuu wa shule za sekondari katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro
Matiro aliwasisitiza wakuu hao wa shule kuwachukulia hatua watu wanaowapa mimba wanafunzi na kuhakikisha wanatoa elimu kuhusu madhara ya ndoa na mimba za utotoni. 
Matiro pia aliagiza shule kutunza mazingira kwa kupanda miti na maua sambamba na kuimarisha usafi kwa walimu na wanafunzi 
Kikao kinaendelea
Mwenyekiti wa wakuu wa shule za sekondari halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Leonard Laurent akisoma risala kwa mgeni rasmi katika kikao hicho, Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro
Kaimu Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Stewart Makali ambaye ni afisa elimu sekondari wa halmashauri hiyo akizungumza katika kikao hicho. Alisema halmashauri hiyo inakabiliwa na upungufu wa viti na meza 3000 katika shule za sekondari.

Katibu wa Chama cha Walimu wilaya ya Shinyanga Victoria Laurent akizungumza kwenye kikao hicho na kuwataka walimu hao wakuu kuhakikisha wanajenga vyumba vya kujistiri kwa wanafunzi wa kike.

Katibu wa Chama cha Walimu Mkoa wa Shinyanga Francis Mbonea akizungumza kwenye kikao hicho na kuwataka walimu wakuu kujituma kufanya kazi kwa bidii na kuondoa matokeo yenye sifuri shuleni kwao ili kuonyesha hamasa kwa serikali na hatimaye kushughulikia matatizo yao ikiwemo kuwalipa madeni na kuwapandisha madaraja

Picha zote na Kadama Malunde na Marco Maduhu - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527