ASKOFU KAKOBE AMUOMBA RADHI JPM KAULI YA "ANA FEDHA KULIKO SERIKALI"


ASKOFU wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship, Zachary Kakobe amemuomba radhi Rais John Magufuli kutokana na kauli yake kuwa yeye (Kakobe) ana fedha kuliko Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Kichere amesema leo jijini Dar es Salaam kuwa, Januari 24 mwaka huu, Askofu Kakobe aliandika barua kwa Rais Magufuli kuomba radhi.

Amesema, TRA imechunguza kauli ya Kakobe na kubaini kuwa hana akaunti wala fedha kwenye taasisi yoyote ya fedha nchini.

Kichere amesema, uchunguzi huo umebaini kuwa, Kakobe ni mmoja wa wasimamizi wakuu wa akaunti ya kanisa hilo iliyopo Benki ya NBC.

Kwa mujibu wa Kichere, akaunti hiyo ina shilingi 8,132,100,819.00 zilizotokana na sadaka, zaka, na michango ya waumini na kwamba, kwa mujibu wa sheria, fedha hizo hazitozwi kodi.

“Aidha, wakati uchunguzi huo ukiendelea, mnamo tarehe 24.01.2018 Askofu Kakobe aliandika barua kwa Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuomba radhi kutokana na kauli yake ya kebehi pamoja na matamshi yake ya dharau kwamba, ana pesa nyingi kuliko serikali” amesema Kichere.

IMEANDIKWA NA BASIL MSONGO - HABARILEO

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527