Breaking News : DAVID KAFULILA NAYE AJIONDOA CHADEMA


Mwanasiasa maarufu wa Tanzania David Kafulila , pia Mbunge wa zamani wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), ambaye Disemba mwaka jana alijiunga na Chadema, David Kafulila leo Jumatano Novemba 22,2017 ametangaza kujivua uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa kile alichosema hana imani na vyama vya upinzani kama jukwaa salama la kupambana na ufisadi nchini Tanzania.

Kafulila amejiondoa CHADEMA na baada ya maamuzi hayo ameeleza sababu kwamba kwa sasa vyama vya upinzani vinaonekana kupigwa ganzi na kupooza katika juhudi zake za kupambana na ufisadi na ghafla ufisadi siyo agenda kuu tena ya vyama vya upinzani tena. 

Kafulila ametoa waraka wa kujivua uanachama wa Chadema.

Katika waraka huo, Kafulila amesema tangu Rais John Magufuli achaguliwe na kukabidhiwa jukumu la kuongoza nchi, vita ya miaka mingi dhidi ya ufisadi imechukua sura mpya.

“Wahusika na watuhumiwa wakubwa wa rushwa ambao walikuwa hawaguswi huko nyuma tunashuhudia wakifikishwa mbele ya vyombo vya sheria. Kutokana na juhudi za kupambana na rushwa na ufisadi zinazoendelea nchini,juhudi hizi zinapaswa kuungwa mkono,” amesema Kafulila.

“Vyama vya upinzani vinaonekana kupigwa ganzi na kupooza katika juhudi zake za kupambana na ufisadi. Ghafla ufisadi sio tena agenda kuu ya vyama vya upinzani nchini, kwa sababu hii, ni wazi kuwa upinzani sio tena jukwaa salama la kuendesha vita dhidi ya ufisadi,” ameongeza.

Kafulila ambaye ni mme wa mbunge wa viti maalum Chadema, Jesca Kishoa amesema "kwa kuwa sina imani tena na upinzani kama jukwaa salama la kupambana na ufisadi, nimeamua kwa hiari na utashi wangu kujivua uanachama wa Chadema kuanzia leo",amesema Kafulila.

“Nitatangaza katika siku za hivi karibuni jukwaa jipya la harakati zangu dhidi ya ufisadi. Nawatakia safari njema waliobaki ndani ya Chadema kwa kile wanachokiamini”,amesema.

Kafulila aliyekuwa mbunge 2010-2015 alitikisa kwenye mapambano ya sakata la ufisadi wa mabilioni ya akaunti ya Tegeta Escrow iliyoitikisa serikali katika utawala wa Rais mstaafu Jakaya Kikwete ametangaza uamuzi huo leo Novemba 22,2017.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527