Video: MSIGWA,LEMA WATEMA CHECHE,WAFUNGUKA MAKUBWA WAKIHOJIWA KUHUSU TUNDU LISSU

Wabunge wawili wa Chadema wametumia mahojiano nje ya nchi kuzungumzia matatizo ya Tanzania wakisema hayawezi kumalizwa na mtu mmoja bali kwa mifumo imara ya mihimili ya Mahakama, Bunge na Serikali.

Wakizungumza katika mahojiano na Kituo cha Televisheni cha KTN cha Nairobi, Kenya  jana Jumapili walisisitiza umuhimu wa kuwa na Katiba Mpya ili kuipa nguvu mihimili hiyo.

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alisema ufisadi ambao Rais John Magufuli anaushughulikia sasa ulifanywa na watendaji waliokuwa chini ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Alisema chama hicho kimeongoza nchi tangu Tanzania ilipopata Uhuru, hivyo ufisadi huo ulifanywa na viongozi waliokuwa chini ya chama hicho.

“Ili tuwe na mfumo wenye nguvu tunatakiwa kubadilisha Katiba ili tuwe na Mahakama na Bunge huru,” alisema.

Lema alisema kumtegemea mtu mmoja hakuwezi kuleta mafanikio kama ambayo yamefikiwa na Kenya.

Alisema Katiba ikibadilishwa na kuwa na vipengele mbalimbali, vikiwemo vya kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi na kumshtaki Rais akitoka madarakani Tanzania itakuwa imepiga hatua.

Alisema mabadiliko ya Katiba nchini Kenya si tu yataisaidia katika siasa bali katika kukuza uchumi wao.

“Uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Kenya kufuta matokeo ya Rais si tu yatawasaidia kisiasa bali yatajenga imani hata kwa wawekezaji,” alisema.

Alisema wawekezaji wataongezeka nchini Kenya kwa sababu wanakuwa na imani na Mahakama.

Kwa upande wake, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alisema Rais ana nguvu kuliko mihimili mingine na amekuwa akitoa maelekezo kwa mihimili hiyo.

“Bunge la Tanzania limetekwa na Serikali, wenzetu CCM wako wengi kuliko sisi wapinzani, wakikaa kwenye Party Caucus (vikao vya chama) yao wanaamua mambo yenye manufaa kwa chama chao,” alisema.

Alisema madhara ya wabunge wa CCM kufanya uamuzi wenye manufaa kwa chama hayawaathiri wapinzani tu, bali Watanzania kwa jumla.

Wabunge hao wako jijini Nairobi kumjulia hali Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu aliyelazwa katika Hospitali ya Nairobi baada ya kupigwa risasi Septemba 7 mwaka huu akiwa nyumbani kwake Area D, mjini Dodoma.


==>Wasikilize hapo chini

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527