TUNDU LISSU ATANGAZWA KUWA MWANASIASA SHUJAA AFRIKA


Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Tundu Lissu, ametangazwa katika kongamano la kimataifa lililofanyika jijini Lagos, nchini Nigeria, kuwa ndiye mwanasiasa kiongozi katika kutetea matumizi mazuri ya raslimali za taifa lake,anaandika Jabir Idrissa.

Wanakongamano waliokusanyika kujadili amani duniani, wamesema: “Lissu ni kielelezo kizuri cha kiongozi mwenye maadili na shujaa wa haki za binadaamu… mpenda haki na mwanasiasa mkweli anayestahiki kuombewa na wapenda amani hata kufikia kuwa rais katika nchi yake.”

Kwa ujasiri wake katika kukataa dhulma na kuitumia vema fani ya sheria katika kusimamia raslimali za taifa lake, wanakongamano wamesema, “mamilioni ya vijana duniani kote wameanza kuomba kusoma fani ya sheria vyuoni baada ya mitandao ya kijamii zaidi ya 11,000 kuripoti habari zake kwa muda wa siku 11 mfululizo kuliko habari za rais yoyote duniani.”

Taarifa zilizofikia MwanahalisiOnline kutoka Nigeria, zimesema hatua hiyo imefikiwa kwenye kongamano lililomalizika jana likishirikisha vijana wasomi wa Kikristo kutoka vyuo vikuu 283 vya Afrika, Marekani, Asia na Ulaya waliokubaliana kuwa Lissu ni kielelezo kizuri cha kiongozi mwenye maadili na shujaa wa haki za binaadamu.

Profesa Bigs Ezziel kutoka Marekani ambaye katika kongamano hilo la siku tano alifundisha mada ya HAKI, ameonya kuwa nchi nyingi za Afrika bado hazijui thamani ya haki ambayo ndiyo tunu nguzo kuu ya amani na demokrasia.

Akimzungumzia Lissu, Prof. Ezziel alisema wamefuatilia kwa karibu habari za mwanasiasa huyo na kuridhika kuwa ni mtu wa pekee kwa kusema ukweli. “Kwenye Balozi zetu wamekuwa wakituletea mambo yote pale Tanzania bila ya shaka anatakiwa apewe tuzo maalum ili kuwachochea vijana wa kizazi hiki kukataa dhulma.”

Prof. Ezziel ameshauri wasomi wa sheria katika nchi za Afrika kumualika Lissu kwenye vyuo vyao ili atoe elimu itakayowezesha wasomi kuielewa fani ya sheria kwa mapana yake kuliko ilivyo sasa kukikosekana tija hasa ya wanasheria katika nchi zao.

“Ni muhimu tutambue kuwa HAKI ni nguzo muhimu kwa amani, upendo na maendeleo. Mwenyezi Mungu anajitambulisha waziwazi kuwa yu Mungu wa haki… inasikitisha wanasiasa wengi barani Afrika wapo kama mafisi kwa kutamani madaraka badala ya kutamani kumtambua Mungu kwa kufanya yale yanayojenga jamii zao.

“Badala yake wanatumia siasa za kugawa wananchi huku wakitumia nguvu za dola kuharibu amani na utulivu katika nchi zao. Tanzania inakwenda vibaya kutokana na wanasiasa kutoenenda katika kuonesha ni kielelezo cha maadili kama alivyokuwa Mwalimu Nyerere ambaye hakutaka kujilimbikizia mali wala kupenda kutumia nguvu za dola kuonea wananchi,” alisema.

Amehimiza viongozi wa kiroho barani Afrika kumuomba Mwenyezi Mungu kulisaidia taifa la Tanzania ili kulinusuru na balaa linaloweza kutokea kutokana na maongozi yanayokiuka haki za binaadamu huku wakimuombea Lissu, ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) baraka ili kutimiza ndoto yake ya kuona maliasili na raslimali za Tanzania zinanufaisha Watanzania.

Amesema Afrika inahitaji mabadiliko makubwa kisiasa, tofauti na siasa zinazoshuhudiwa zama hizi kwa marais kunogewa na madaraka hata kujifanya Miungu watu. Waruhusu mawazo ya wengi kutawala badala ya kauli ya mtu mmoja kuongoza taifa la mamilioni ya watu. Huko ni kumkataa Mwenyezi Mungu ambaye humsikiliza na kumlisha kila mtu na kila ndege wa angani.

Prof. Ezziel, mwanasheria na mshauri wa sheria kwenye vyuo vikuu 17 vya Palestina, Djibouti, Ghana, Marekani na Jerusalem, amepongeza wanasheria wa Tanzania kwa kumchagua Lissu kuwa rais wa jumuiya ya wanasheria ya Tanganyika. Uamuzi wao wakati wa mkutano mkuu wa Tanganyika Law Society (TLS), amesema umewapata kuheshimika duniani.

Kadhalika, Lissu ametajwa na Dk. Marucus Bahod na Dk. Chris Zulu kuwa “mwanasiasa wa mfano katika karne hii” ambaye ameifundisha dunia umuhimu wa kusimamia haki na sheria na kuifanya taaluma ya sheria kung’aa kwa muda mfupi kiasi cha kusababisha macho yote ya wanazuoni duniani kuiangalia Tanzania kwa kumfuatilia Lissu.

“Ni mwanasheria anayejiamini kutetea matumizi mazuri ya raslimali na maliasili za taifa lake bila ya kujali nguvu kubwa inayotumika na serikali kumkatisha tamaa… mwanasiasa anayeweza kuiongoza Tanzania kwa uwezo wake wa kimaadili na kuitafsiri sheria kwa faida ya Watanzania wote.

“Ni mfano mzuri kwa wanasheria wengine Afrika ambao wanakuwa wazito kusimamia matumizi ya manufaa ya maliasili katika nchi zao na hivyo kuzinyima fursa za maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Kutokuwa mbele katika kutetea maliasili za mataifa ya Afrika kunachangia kuua demokrasia, utawala wa haki na sheria,” alisema.

Madaktari hao walisema ni vema wanaotafuta uongozi wa kisiasa barani Afrika wawe watu wema na kamwe wasiruhusu watu wenye visasi kupewa dhamana ya uongozi kwani wakishapata madaraka, huzalisha chuki na fitna katika jamii badala ya maendeleo.

Askofu William Muller kutoka Ujerumani, aliongoza dua ya kuiombea Kenya kuendelea na amani wakati na baada ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi huu. Nazo nchi za DR Congo, Tanzania, Afrika Kusini, Msumbiji, Ghana, Nigeria, Uganda, Burundi na Gabon zimeombewa ili zirudi kwenye maendeleo makubwa ya kiuchumi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527