RAIS MAGUFULI AMTEMBELEA AFISA WA JESHI ALIYEPIGWA RISASI DAR


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 12 Septemba, 2017 ametembelea hospitali ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Lugalo, Jijini Dar es Salaam na kumjulia hali Meja Jen. Mstaafu Vincent Mritaba aliyelazwa hospitalini hapo baada ya kushambuliwa na watu wenye silaha wakati akiingia nyumbani kwake Ununio, Kinondoni Jijini Dar es Salaam.


Meja Jen. Mstaafu Mritaba alishambuliwa kwa risasi jana tarehe 11 Septemba, 2017 majira ya mchana na kisha kukimbizwa katika hospitali ya Jeshi Lugalo kwa matibabu.


Mkuu wa kituo cha tiba cha hospitali hiyo na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo Brigedia Jenerali Paul Massawe amemueleza Mhe. Rais Magufuli kuwa Meja Jen. Mstaafu Vincent Mritaba anaendelea vizuri baada ya madaktari kufanikiwa kutoa risasi alizopigwa mkononi, kiunoni na tumboni.


Meja Jen. Mstaafu Mritaba amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumjulia hali na kumuombea dua ili apone haraka.


Mhe. Rais Magufuli aliyeongozana na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jen. Venance Mabeyo pia ametembea wodi ya majeruhi na kuwajulia hali wagonjwa wanaotibiwa katika wodi hiyo na baadaye akawasalimu wananchi waliofika hospitali hapo kwa ajili ya kupata matibabu.


Mhe. Dkt. Magufuli amewapongeza Madaktari wa hospitali ya jeshi Lugalo kwa huduma za matibabu wanazotoa kwa askari na wananchi wengine na amewahakikishia kuwa Serikali itaendelea kufanyia kazi changamoto mbalimbali zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
12 Septemba, 2017

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527