MUME AUA MKE WAKE KISHA NAYE KUJIUA MWANZA



Mume na mke wamefariki dunia katika kijiji cha Mwagiligili mkoani Mwanza baada ya mume Kwilokeja Boniphace (35) kumuua mkewe Shija Luchagula (30) kwa kumpiga na kumnyonga kisha naye kujinyonga kwa kile kinachosemekana kuwa ni wivu wa mapenzi. 


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema mtuhumiwa wa mauaji hayo alikuwa akimtuhumu mkewe kuwa anatoka kimapenzi nje ya ndoa hali iliyopelekea ugomvi kati yao.

"Inasemekana kuwa mtuhumiwa wa mauaji hayo alikuwa akimtuhumu mkewe kuwa anatoka nje ya ndoa hali iliyopelekea kuzuka kwa ugomvi wa mara kwa mara baina yao. Inadaiwa kuwa kabla ya tukio hilo la mauaji kutokea siku hiyo mtuhumiwa aliamka asubuhi na kufagia uwanja wa nyumba yao kama mtego wa kubaini watu wanaokuja hapo nyumbani kwake, kisha alikwenda kwenye shughuli zake za kawaida", ilisema taarifa ya Msangi  

"Inadaiwa kuwa baada ya muda mchache kupita mtuhumiwa alirudi nyumbani, ndipo akiwa hapo nyumbani kwake aliona matairi ya baiskeli katika uwanja wa nyumba yake ndipo ulizuka ugomvi kati yake na mkewe huku akimtuhumu mkewe kuwa alikuwa si mwaminifu katika ndoa hapo nyumbani kwake na kupelekea kumpiga mkewe hadi kumuua na yeye mwenyewe kujinyonga hadi kufa" ,iliongeza

Aidha taarifa ya Kamanda Msangi imesema kuwa miili ya wanandoa hao imekabidhiwa kwa ndugu zao kwa ajili ya mazishi.
NA GERALD KITALIMA -MWANZA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527