MAALIM SEIF : TUNDU LISSU HAJAPOTEZA MUELEKEO,AKILI YAKE IPO TIMAMU

Katibu  Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, ameeleza maendeleo ya afya ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), baada ya kumtembelea hospitalini Nairobi, Kenya.

Akihojiwa na Redio ya Idhaa ya Kiswahili Deutsche Welle (DW) ya Ujerumani jana, Maalim Seif alisema Lissu anaendelea vizuri na hajapoteza mwelekeo.

“Jana (juzi) nilimtembelea Lissu na nilipata moyo sana, kwa kweli anaendelea vizuri ukizingatia mtu ambaye alipigwa risasi zaidi ya 30, anapata nafuu haraka haraka.

“Bado hajapoteza mwelekeo akili yake ipo timamu, ametuhakikishia haya yaliyotokea hayatamrudisha nyuma katika kuwatetea wanyonge.

“Anazungumza vizuri, yuko makini sana anajua anachokisema na mimi nimepata moyo jinsi nilivyomuona,” alisema Maalim Seif.

Alisema kutokana na mambo yanayoendelea nchini, lazima kuwapo na mjadala wa  taifa   kuona tumekosea wapi na kujirekebisha.

“Mambo kama haya kutokea Tanzania ni jambo ambalo kila Mtanzania lazima aingiwe na wasiwasi kwa sababu hakuna hata mmoja na hasa mwanasiasa ambaye ana usalama wa maisha yake.

“Kama taifa tuzungumze kuona tumekosea wapi na kujirekebisha,” alisema.

Kuhusu uchunguzi wa tukio hilo, alisema hata kama vyombo vya dola vya ndani vitafanya  si aibu kwa nchi kutafuta msaada kwa wengine.

“Yako mambo mengine yaliyotokea huko nyuma na bado hatujaaambiwa yalikwenda vipi, tunaambiwa tu uchunguzi unaendelea. Ni vizuri wananchi waone matokeo ya uchunguzi huo…si aibu kwa nchi kutafuta msaada kwa wengine,” alisema.

Lissu alipigwa risasi  zinazokadiriwa kufikia 32, Septemba 7, mwaka huu, alipokuwa akirejea nyumbani kwake Area D mjini Dodoma baada ya kutoka kuhudhuria kikao cha Bunge na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527