SUMAYE ATINGISHWA TENA,RAIS MAGUFULI ARIDHIA APOKONYWE SHAMBA LAKE

Waziri Mkuu wa mstaafu, Frederick Sumaye ameingia matatani tena baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero kumpokonya shamba lake lenye ukubwa wa ekari 326 kwa madai ya kutoendelezwa huku ikisema Rais John Magufuli ameridhia hatua hiyo.


Hili ni shamba la pili Sumaye kunyang’anywa baada ya ekari 33 zilizopo eneo la Mabwepande kuchukuliwa Novemba mwaka jana huku Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi akisema Serikali ilifikia uamuzi huo baada ya kiongozi huyo mstaafu kushindwa kuliendeleza kama notisi ya siku 90 ilivyoeleza.


“Oktoba 28, mwaka huu, Rais John Magufuli alibatilisha hati ya kumiliki ardhi ya shamba namba 3,074 lililopo Mabwepande. Shamba hilo lilikuwa na hati namba 53086. Jina la mmiliki lililoandikwa katika hati ni Frankline Sumaye,” alisema Hapi.


Jana, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mvomero, Frolent Kyombo alisema Rais Magufuli amekubali kufutwa kwa umiliki wa shamba hilo kupitia ilani ya ubatilisho ya Mei mwaka huu.


Kabla ya kupokonywa shamba hilo, Kyombo alisema Sumaye alipewa notisi ya siku 30 iliyomtaka kueleza sababu za kutoendeleza matumizi ya shamba hilo kwa shughuli za kilimo kama lilivyosajiliwa lakini hakutoa sababu zilizoweza kushawishi kutofanyika kwa mabadiliko hayo.


“Hatua ya pili, tukatoa ilani ya ubatilisho wa shamba hilo, kuna maelezo alitoa lakini tuliona hayakuwa na uzito, tukayatupilia mbali, shamba hilo alikuwa anaendesha shughuli za kilimo pamoja na ufugaji. Alikuwa anatumia asilimia 15 hadi 20 tu ya shamba lote,” alisema Kyombo.


Alisema mbali na kutumia sehemu ndogo huku nyingine ikiwa haitumiki, Mwenyekiti huyo wa Chadema Kanda ya Pwani alikuwa amekiuka Sheria ya Mipango Miji, namba 8 ya mwaka 2007 pamoja na Sheria ya Ardhi namba 4 ya 1999.


“(Sumaye) alitakiwa kutumia shamba hilo kwa ajili ya kilimo tu na siyo kwa shughuli nyingine za ufugaji, hilo ni kosa kwa mujibu wa sheria hizo. Kwa hiyo mchakato umeashaanza wa kuligawa shamba hilo kwa wananchi na tunategemea miezi minne ijayo tutakuwa tumemaliza taratibu zote,” alisema.


Desemba 15, 2015, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi alitangaza kiama kwa watu wanaomiliki mashamba bila kuyaendeleza huku wakiyatumia kama dhamana ya kukopea fedha benki.


Akizungumza kwa mara ya kwanza baada ya kuteuliwa na Rais Magufuli, alisema kuna watu wamehodhi mashamba makubwa lakini hawayaendelezi, hawayalipii kodi na mbaya zaidi, wanayatumia kukopa fedha benki.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527