MSICHANA AUAWA, AFUNIKWA MFUKO WA SANDARUSI KISHA KUZIKWA KWENYE SHIMO KISA KAGOMA KUOLEWA RUKWA

NB-Picha haihusiani na habari hapa chini
****

MSICHANA asiyefahamika jina wala umri wake ameuawa kwa kipigo na kisha mwili wake kufukiwa kwenye shimo huku ukiwa umewekwa kwenye mfuko wa sandarusi.Mwandishi wa Malunde1 blog,Walter Mguluchuma anaripoti.



Tukio la mauaji ya msichana huyo lilitokea Julai 18 majira ya saa mbili asubuhi katika kijiji cha Kate kata ya Kate wilayani Nkasi mkoani Rukwa ambapo uvumi ulienea kijijini hapo kuwepo kwa mauaji na baada ya uchunguzi ndipo lilipogundulika shimo na kufukiwa porini umbali wa kilomita moja kutoka kijijini.

Kamanda wa polisi mkoa wa Rukwa George Kyando alisema  baada ya kulifukua shimo hilo walikuta mwili wa mwanamke huyo na baada ya uchunguzi wa kidaktari mwili wa marehemu ulikutwa na majeraha matatu kichwani ya kukatwa na kitu chenye ncha kali kinachodhaniwa kuwa ni panga.

Kamanda Kyando alidai kuwa marehemu alifika kijijini hapo akitokea jijini Dar es salaam ambapo inadaiwa ni mwanafunzi na kufika kwa mwenyeji wake aliyejulikana kwa jina la Samwel Selemani na kumtambulisha kwa jirani zake kuwa ni mpenzi wake.


"Waliendelea kuishi pamoja baada ya muda kijana huyo alitoweka nyumbani na kuelekea kusikojulikana na mwanamke mwenyewe hakuonekana na kuwa siku chache za nyuma kulitokea ugomvi kati mwanaume na marehemu ambapo mwanamke alikuwa akiomba nauli ya kurudi jijini Dar es salaam kwa madai kuwa anataka arudi shule lakini mwanaume ambaye ni mtuhumiwa alikataa kuitoa nauli hiyo akidai kuwa hataki mpenzi wake huyo aondoke",alieleza Kamanda huyo.

"Baada ya mvutano wa muda mrefu ndipo mtuhumiwa alidai kumuua mapenzi wake huyo na kuufukia mwili wake kwani hakuwa tayari mwanamke huyo aondoke kwani yeye alitaka waanze kuishi pamoja wakati mwanamke huyo alikuwa hayupo tayari kwa madai kuwa ni mwanafunzi.

Marehemu hakuweza kutambulika na kuzikwa eneo la tukio,huku mtuhumiwa aliyedaiwa kuwa ni mpenzi wake hajapatikana mpaka hivi sasa na jeshi la Polisi linaendelea kumtafuta na iwapo atakamatwa afikishwe mbele ya sheria.

Na Walter Mguluchuma-Malunde1 blog Nkasi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527