MKE WA MTU AJIUA KWA KUJINYONGA KISA AMESHINDWA KUREJESHA PESA ZA MKOPO SHINYANGA

Mkazi wa mtaa wa Tambukareli kata ya Ndembezi katika manispaa ya Shinyanga Sarah Bundala (55) amejiua kwa kujinyonga kutokana na kile kilidaiwa kuwa ameshindwa kurejesha fedha za mkopo  alizomdhamini rafiki yake ambaye ametoroka.

Pesa alizotoroka nazo rafiki huyo hazijulikani idadi yake.


Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga ACP Muliro Jumanne Muliro alithibitisha kutokea kwa tukio hilo lililotokea jana Ijumaa Julai 14,2017.



Akizungumzia tukio hilo mume wa marehemu Laurent Mabina, alisema wakati akiwa bado kazini majira ya saa 9 mchana alipigiwa Simu na mke wake akimuomba Shilingi 40,000/- akamjibu kuwa anarejea nyumbani muda huo na akifika wataangalia cha kufanya lakini alipofika akakuta mkewe amejinyonga.


“Mke wangu alishawahi kukopa fedha akashindwa kulipa nikalazimika kulipa na kumuonya kwamba asijiingize tena kwenye masuala ya mikopo,huenda sababu ya mke wangu kujinyonga ni ile hofu kuwa nikirudi nyumbani nitakuja kugombana naye sababu nilishamkataza mambo ya mikopo" alisema Mabina.

Habari kutoka eneo la tukio zinasema kuwa marehemu alikuwa amedhamini rafiki yake apate mkopo lakini rafiki huyo akatoroka na pesa za mkopo ambazo kiasi chake hakijafahamika hivyo deni la mkopo kuwa lake huku wanaodai wakisema watafika nyumbani kumfirisi.

Akisimulia kuhusu tukio hilo rafiki yake Mariam Mgaya,aliiambia Malunde1 blog kuwa,majira ya saa nane mchana siku ya tukio alimuita ili amsindikize wakatafute pesa za kukopa, ili akarejeshe marejesho lakini walivyozunguka na kukosa ndipo akamshauri ampigie simu mume wake amsaidie kiasi hicho cha pesa anachohitaji akagoma kufanya hivyo.

Alisema baada ya kushauriana wapi watapata pesa na kukosa majibu, marehemu alimwambia anataka kwenda nyumbani kulala kwanza na ikifika majira ya saa 10 arudi kumuona na hata watu wakimuuliza yuko wapi awaambie amelala nyumbani kwake asiwafiche na ilipofika muda huo akapokea taarifa rafiki yake amejinyonga.

Matukio ya watu kuchukua uamuzi wa kujiua yameanza kukithiri katika manispaa ya Shinyanga ambapo ndani ya miezi miwili,Juni na Julai mwaka huu,hili ni tukio la tano,matukio ambayo yanatokea katika kata ya Ndembezi na Ngokolo ambazo zinatenganishwa na barabara ya Mohammed Trans mjini Shinyanga.

Na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527