MAMBO MANNE YANAYOATHIRI MALEZI YA MTOTO

KATIKA malezi ya mtoto ya kila siku zipo changamoto ambazo zinachangia kumjenga katika makuzi na nyingine zinaweza zikamuharibu.

Changamoto zote hizi zinapaswa kutatuliwa ili mtoto aweze kukua katika utaratibu mzuri unaoleweka.

Makuzi ya mtoto/watoto ni jukumu la muhimu sana kwa mzazi yo yote katika jamii.Katika tafiti mbalimbali za kisayansi makuzi anayopata mtoto kuanzia umri wa miaka sifuri hadi 12 yanaakisi tabia atakayokuwa nayo katika utu uzima wake.

Kutokana na hali hiyo kuna mambo manne ambayo mzazi unapaswa kuyaangalia ili kuepuka kuathiri makuzi ya mtoto.

Moja ni kumuaibisha,hatua za kinidhamu unazochukua dhidi ya mtoto wako huathiri malezi yake.

Wataalam wa malezi ya watoto wanashauri malezi yetu yawe shirikishi kwa maana ya kwamba kila unapomkataza mtoto kufanya jambo fulani kama vile kutukana watu, utoro shuleni, ugomvi n.k ni vizuri zaidi ukawa unamfahamisha ni kwa nini haifai kufanya jambo fulani.

Lengo ni kumpatia nafasi ya kuhoji/kutafakari/kuelewa badala ya kumshurutisha tu kutekeleza maagizo.

Kwa kufanya hivyo, unampa uwezo wa kupambanua, kuelewa na kujiamini katika maamuzi mbalimbali. Pia hatua kali za kinidhamu kama vile kumchapa mtoto zinaweza kusababisha hofu kwa watoto wako, ambayo huathiri uwezo wao wa kuwasiliana na wewe, walimu na wezake.

Hata hivyo, pia haitakiwi kuwa mpole mno kwa sababu watoto wanaweza kuendelea kwa wakosefu wa nidhamu na kuathiri mwenendo wao katika jamii na shuleni.

Jambo la pili ni mazingira,neno mazingira kwa tafsiri fupi ni vitu vyote vinavyotuzunguka hewa, miti, majengo, watu, wanyama, shule, nyumba za ibada .n.k.

Mazingira ya mtoto yanaathiri ya moja kwa moja kwa mtoto hasa ya nyumbani na shuleni. Muda mwingi wa makuzi ya watoto hutumika nyumbani na shuleni.

Mtoto anayetoka kwenye nyumba ambayo wazazi wake wako katika hali ya ugomvi kila mara, umasikini, utajiri n.k. mambo hayo umuathiri moja kwa moja kimtazamo wa kimaisha.

Jambo la tatu la kuangalia ni mawasiliano,mtoto anapaswa kushirikishwa katika baadhi ya maamuzi ya kifamilia kama vile masuala ya chakula, vinywaji, maongezi n.k.

Ninaposema kushirikishwa katika suala ya chakula ni katika hali ya kujenga tabia ya ushirikishwaji na kumpa uhuru wa maamuzi kumuuliza mtoto leo unataka kula nini mama/baba ni kuonyesha kuthamini mawazo yake.

Pia katika maongezi nina maana mtoto akisema jambo lolote ni muhimu kumsikiliza na siyo vizuri kumpuuza au kumkaripia kwamba anapiga kelele.

Tabia hiyo, itamsaidia kwa kumpatie uwezo wa kujieleza na kujisikia kuthaminiwa na wazazi wake.

Mbali na hayo mfumo wa malezi pia unaweza kumjenga mtoto wako au kumuharibu.

Kuweka ratiba ya kukaa na watoto na kuongea nao na kusikiliza mawazo hayo huwajengea hali ya kujisikia kuathaminiwa na kupendwa na wazazi/walezi na hivyo kuwaongezea furaha na amani.

Pia tabia hii huwajengea hali ya kujiamini na uhuru wa kueleza hisia zao nyumbani na shuleni bila hofu kwa sababu ya Imani ya kupendwa imejengwe kwenye akili zao.

Wazazi tuna jukumu kubwa katika kujenga watoto wetu kisaikologia katika akiwa mdogo,kumjenga ukubwani ni vigumu kwakuwa akili inakuwa imeshakomaa.

NA AZIZA MASOUD-MTANZANIA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527