Ushirikina! MAPEPO YAVAMIA WANAFUNZI SHULE YA IMESELA SHINYANGA VIJIJINI,SHUHUDIA HAPA YAKIWATESA MBELE YA MKUU WA WILAYA

Ushirikina!! Ndivyo unavyoweza kusema…Wanafunzi wa shule ya sekondari Imesela iliyopo kata ya Imesela wilaya ya Shinyanga(Shinyanga vijijini) mkoa wa Shinyanga wamekumbwa na mapepo yanayowafanya waanguke na kupiga kelele wakitamka maneno yasiyoeleweka huku wakiwataja baadhi ya watu wanaofanya ushirikina huo.

Tatizo la wanafunzi wa kike kuanguka na kupiga kelele shuleni hapo lilianza mwezi Januari mwaka huu lakini hali hiyo ilikithiri Machi 20 mwaka huu ambapo wanafunzi takribani 16 wakianguka na kuanza kutamka maneno wakiwataja baadhi ya watu wanaofanya ushirikina shuleni hapo. 

Wanafunzi hao wamekuwa wakiugua ugonjwa usiojulikana wa kuanguka na kupoteza fahamu na kutamka maneno yasiyoeleweka kitendo ambacho kinahusishwana imani za kishirikina.

Inaelezwa kuwa mapepo hayo huwasumbua hasa wanafunzi wa kike mara tu wanapofika shuleni majira ya saa moja na nusu asubuhi mpaka saa tano lakini pia kuanzia saa saba mchana mpaka saa tisa alasiri wanapotawanyika kurudi majumbani mwao.

Aidha inadaiwa kuwa wanafunzi hao mara tu wanapopatwa na mapepo hayo huanguka na kupiga kelele huku wakigaragara na kuwarushia ngumi wanafunzi wenzao.

Shule ya sekondari Imesela iliyoanzishwa mwaka 2006 ina jumla ya wanafunzi 252 kati yao 130 ni wa kike na 122 ni wa kiume huku walimu wa wakiwa 14 ambapo mmoja pekee ni mwanamke.
Walimu wa shule hiyo wanasema vitendo hivyo vya kishirikina vinaathiri utaratibu wa vipindi vya wanafunzi hao ambapo wamekuwa wakitumia muda mwingi kusaidiana na wanafunzi wa shule hiyo kuwasaidia wanafunzi wanaopatwa na majanga hayo.

Mkuu wa shule hiyo Seleman Kalavina amesema mauza uza huanza kila siku asubuhi pindi tu wanapofika shuleni hali inayowafanya wanafunzi kupoteza muda wao wa masomo huku ikiwakatisha tamaa walimu wa shule hiyo kufundisha na kutamani kuhama shule hiyo.

Mratibu wa Elimu kata ya Imesela Julius Wamba amesema wamefanya jitihada za kuwaita viongozi wa dini kufika shuleni na kufanya maombi ili kumaliza tatizo hilo lakini mara tu wanapoondoka tatizo hujirudia. 

Kutokana na mauza uza hayo,leo Jumatano Machi 29,2017 mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama amelazimika kufika katika shule hiyo na mara baada tu ya kufika mashetani yakawapanda wanafunzi hao. 

Mkuu huyo wa wilaya amelazimika kuifunga shule hiyo kwa muda siku mbili ili viongozi na wananchi wa eneo hilo wakutane naye siku ya Ijumaa wiki hii ili kujadili namna ya kumaliza tatizo hilo. 

“Serikali haiamini ushirikina,hivi vitendo mnavyofanya siyo vizuri,watoto wanashindwa kusoma kwa sababu ya ushirikina wenu,tena mnawatesa watoto wa kike tu,hamtaki wasome mnataka kuwaoa? Si mkarogane wenyewe muwaache watoto wasome,nataka siku ya Ijumaa wote tukutane hapa tujadili namna ya kuwasaidia wanafunzi hawa”,alisema Matiro. 

Malunde1 bog imeshuhudia wanafunzi hao wakianguka ovyo na kutamka maneno ya ajabu ajabu huku wengine wakitaka kupigana mpaka pale wanafunzi wenzao wanapoamua kuwakamata na kuwafunga na nguo mikononi na miguuni ili wasikimbie kisha kuanza kuwafanyia maombi.

Mwandishi wetu Kadama Malunde aliyefika shuleni hapo anasema wanafunzi na walimu wamekuwa wakigeuka kuwa wachungaji na kuanza kuwaombea wanafunzi hao.Tazama picha hapa chini

Wanafunzi wa shuleya sekondari Imesela wakimsaidia mwanafunzi mwenzao aliyepandwa na mapepo leo Jumatano Machi 29,2017-Picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog
Heka heka ya mapepo ilianza baada ya msafara wa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro aliyekuwa ameambatana na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Shinyanga huku ikielezwa kuwa mapepo hayo hufanya hivyo kuonesha kuwa yapo kila anapofika mtu yeyote kukabiliana nayo
Wanafunzi wakimsaidia mwanafunzi mwenzao aliyepandwa na mashetani katika shule ya sekondari Imesela
Mwalimu akiwaombea wanafunzi wake waliopandwa na mapepo
Wanafunzi wakiwafanyia maombi wanafunzi wenzao waliangushwa na mapepo.


Zoezi la kusaidia wanafunzi waliopatwa na mapepo likiendelea

Mkuu wa shule ya sekondari Imesela Seleman Kalavina akieleza namna wanafunzi wanavyoteswa na mapepo shuleni hapo
Katibu tawala wa wilaya ya Shinyanga Boniface Chambi akimkaribisha mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro ili azungumze na baadhi ya wananchi waliofika katika shule ya sekondari Imesela 
Heka heka ya mapepo/mashetani ikiendelea 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na baadhi ya wakazi wa Imesela 
Wananchi wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na wananchi wa Imesela ambapo kutokana na mwitikio mdogo wa wananchi alitangaza kufanya mkutano mwingine siku ya Ijumaa wiki hii ambao utahudhuriwa na viongozi wote ngazi ya kata likiwemo jeshi la jadi sungusungu ili kutatua tatizo hilo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza shuleni hapo
Mkuu wa wilaya akizungumz
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga akizungumza na wananchi wa eneo hilo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527