DC SHINYANGA ATOA MBINU KWA WANAWAKE KUJINASUA NA MFUMO DUME


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro ametoa mbinu kwa wanawake kujinasua na mfumo dume kwa kuachana na tabia tegemezi, ambayo husababisha kukithiri kwa manyanyaso kwao kutoka kwa waume zao.

Amewataka wajikite kwenye vikundi vya ujasiriamali ambavyo vitawaondoa kwenye mfumo huo kwa kujikwamua kiuchumi.

Matiro ameyasema leo mjini Shinyanga wakati wa hafla fupi ya ugawaji baiskeli 36 kwa wawezeshaji elimu ya ujasiriamali kutoka shirika lisilo la kiserikali (Rafiki-Sido ) mkoani Shinyanga linalojihusisha na mradi wa uwezeshaji wa vijana wa kike hususani wanaoishi katika mazingira magumu ili kuwainua kiuchumi.


Matiro amesema matatizo ya manyanyaso kwa wanawake kutoka kwa waume zao husabishwa na wao wenyewe kutokana na kutojishughulisha na biashara mbalimbali na kubaki kuwa tegemezi kwa mme wake na hivyo kuishi kama mtumwa.

“Ili kuondokana na tatizo la mfumo dume ndani ya jamii ni lazima wanawake wajishughulishe na biashara mbalimbali ambazo zitaondoa dhana ya utegemezi,kama mitaji ipo mnatakiwa mjiunge kwenye vikundi vya ujasiriamali ndipo serikali itoe pesa kwenu zile asilimia tano”,amesema Matiro

Aidha amelipongeza shirika hilo la Rafiki kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii hususani kwenye suala la kumtetea mwanamke na kumuinua kiuchumi, huku akitoa wito kwa wanufaika na mradi huo kuyatumia mafunzo hayo vizuri ili kuondokana na hali ya umaskini.

Naye mkurugenzi wa shirika hilo, Geradi Ngong’a amesema mradi huo wa kumwezesha kijana wa kike kiuchumi, ulianza mwaka 2015 na kutarajiwa kuisha 2018 ambapo mpaka sasa wameshaunda vikundi vya ujasiriamali 180 kutoka katika kata 15 za manispaa ya Shinyanga sawa na vijana 3,833 .

Hata hivyo Ngong’a amesema, mradi huo unahusisha vijana wa kike ambao wapo nje ya shule kuanzia miaka 15-24 wakiwemo waliobebeshwa mimba,kuolewa ndoa za utotoni, kuishi maisha magumu kwa kuwapatia elimu ya ujasiriamali pamoja na kuwaunga kwenye vikundi vya vikoba ili wajikwamue kiuchumi.

Kwa upande wake mmoja wa waathirika wa mimba hizo za utotoni Christina Charles ambaye alipata ujauzito mwaka jana mara baada ya kuhitimu elimu ya darasa la saba ,amesema kabla ya kujiunga na shirika hilo alikuwa na maisha magumu, lakini sasa ana uwezo kwa kujihudumia mwenyewe kwa kuuza mboga mboga.

Nao baadhi ya wawezeshaji waliopewa baiskeli hizo Rose Noel na Getruda Ishengoma wamesema baiskeli hizo zitawasaidia kutembelea vikundi hivyo vya ujasiriamali kwa urahisi pamoja na kushauri vijana wengine wa kike kujiunga na shirika hilo ili wapate kujikomboa na umaskini.

Na Marco Maduhu-Malunde1 blog

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika hafla hiyo
Mkurugenzi wa shirika la Rafiki  Geradi Ngong’a akizungumza
Mkurugenzi wa shirika la Rafiki Geradi Ngong’a akizungumza
Baiskeli zikiwa eneo la tukio
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga akikabidhi baiskeli kwa wawezeshaji
Mwezeshaji akijaribu kuendesha baiskeli

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527