ATUMBUKIA GHAFLA KWENYE CHEMBA YA MAJI TAKA YENYE UREFU WA FUTI 12 DAR


Mkazi wa Temeke Mikoroshoni, Miradji Sanyero, jana alipatwa na mkasa wa kutumbukia katika ‘chemba’ ya kupitishia maji taka yenye urefu zaidi ya futi 12, iliyopo eneo la Bakhresa, Tazara, Barabara ya Mandela jijini Dar es Salaam.

Alipatwa na mkasa huo akiwa katika harakati ya kujitafutia maisha, ambapo ghafla alitumbukia katika chemba hiyo iliyokaa vibaya katika mlango mkuu unaotumiwa na magari makubwa wa ofisi za Bakhresa.

Akijojiwa, akiwa mahututi, alisema “Nilikuwa napita jirani huku nikichukua tahadhari nisigongwe na magari yanayoingia na kutoka katika ofisi hizo, ndipo nikajikuta ghafla nimetumbukia ndani ya chemba hii na kuumia kidole cha mkono wa kulia, miguuni na mbavu ambazo sasa zinauma sasa”.

Wafanyabiashara wadogo (machinga) wa eneo hilo, walisema chemba hiyo ni hatari na watu kadhaa wametumbukia katika kipindi cha hivi karibuni. Walidai huyo alikuwa mtu wa tatu.

“Tunaomba Tanroads wafike eneo hili, waone kisha wazibe chemba hii. Kama hawatafanya hivyo, kuna hatari ya kupoteza maisha hasa watoto wadogo ambao uwezo wao wa kuhimili vishindo ni mdogo sana” alisema machinga mmoja, Ali Tematema.

Gazeti hili lilishuhudia baadaye trafiki wakishirikiana na wananchi, wakimsaidia Sanyero kwenda kupanda bajaji kwenda Polisi kuchukua Fomu Namba 3 ili aende hospitali kufanyiwa uchunguzi wa afya yake.
Chanzo-Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527