MREMA AFUNGUKA KUHUSU HALI YA WAFUNGWA NCHINI TANZANIA,AWACHANA ASKARI WANAOBAMBIKIZIA KESI RAIA



Mwenyekiti huyo wa bodi ya parole taifa Augustino  Mrema amewataka wananchi na viongozi wa dini nchini kujitolea kuwalipia wafungwa walioshindwa kulipa faini ili kupunguza msongamano magerezani.


Akizungumza hii leo asubuhi katika kipindi cha Dodoma 42 cha Rasi Fm Radio , Mh. Mrema amesema hivi  sasa magereza yamejaa wafungwa, ambapo wengine hawakustahili kutokana na kutakiwa kulipia faini pekee jambo linalosababisha kuwa na wafungwa wanaoipaisha bajeti pasi na sababu ya kueleweka.

Hata hivyo amemshukuru kwa mara nyingine Askofu mkuu wa Kanisa la Mlima wa Moto, mama Getrude Rwakatare kwa kujitolea kuchangia shilingi milioni 25 kwa ajili ya kuwalipia wafungwa wapatao 78 waliokuwa wakishikiliwa katika magereza mbali mbali ya jijini Dar es salaam.

Akizungumzia kuhusu polisi jamii na kuwabambikizia kesi watu wasio na makosa, Mrema amesema  Polis jamii haipo kisheria kutokana na kutokuwepo na uwazi juu ya muajiri wake, na kudai kuwa hao wapo kinyume na taratibu.

Amesema ni wakati sasa wa watanzania kujitolea kuisaidia serikali katika hilo kama vile wanavyofanya katika janga la tetemeko la ardhi lililotokea Septemba 10 mkoani Kagera ama kama wafanyavyo katika suala la uchangiaji wa madawati kwa shule za sekondari na msingi hapa nchini. 

Hata hivyo mwenyekiti huyo wa Parole amesema kuwa Magereza hapa nchini yamefurika wafungwa na hivi sasa anaangaika napo kuhakikisha anapunguza msongamano, kwa kushughulikia wafungwa walioshindwa kulipa faini na kutakiwa kutumikia kifungo.

”Unakuta mfungwa kashindwa kulipa faini ya sh. 50,000 anafungwa hata miaka miwili au miezi sita, jambo ambalo si sawa” amesema Mh. Mrema . 

“Serikali itabidi imlipe kwa miaka miwili, ikimuhudumia kwa chakula na matibabu,pia wakiwa gerezani hukutana na watu waliokubuhu kwa masuala ya ujambazi na kujikuta hata wasiokuwa majambazi wanafundishwa na majambazi wanaokutana nao humo, hivyo ni kama serikali inafanya biashara kichaa (biashara isiyo na faida)",alieleza

Akizungumza kuhusu kuwasaidia wafungwa wa namna hiyo Mrema amenukuu kifungu kutoka kwenye kitabu kitakatifu cha Mwenyezi Mungu “Biblia” akisema kuwa Ukisoma mathayo 25:31-36 inasema ” nilikuwa kifungoni ukaja kunitazama, nilikuwa uchi ukaja kunivisha,nilikuwa na njaa ukaja kunilisha”.

Amesema kuwa anadhani maneno hayo katika kitabu cha Mathayo yalimvutia sana askofu mkuu wa kanisa la mlima wa moto Dr Getrude Rwakatare.

Amesema kuwa askofu huyo alifanikisha zoezi la kuwalipia faini wafungwa walioshindwa kulipa, ambapo katika hatua hiyo aliwasaidia wafungwa wa jijini dar es salaam kwa kutoa shilingi milioni 25 kuwalipia na kutoka huku wakijutia makosa yao.

Amesema kuwa sasa wamefanikiwa wafungwa hao wapatao 78 kurejea makwao na kuzihudumia familia zao na kuendelea kuzalisha mali.

Ameongeza kuwa serikali ingeendelea kuteseka kwa kuwachunga wafungwa kwa kuwalisha na kuwahudumia huduma nyingine, lakini pia akiongeza kuwa amefanikiwa kuiingizia serikali mapato katika kipindi hiki baada ya kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa parole.

Amewataka pia wananchi kuwachangia wafungwa waliofungwa kwa makosa madogo pamoja na kushindwa kulipa faini kama vile wanavyochangia katika masuala ya madawati na janga la tetemeko la ardhi mkoani Kagera.

Pia amewataka Maaskofu, Wachungaji, Mapadre, Mashehe na watu wa Mungu kwa ujumla kuelekeza macho yao kwa watu walio magarezani hasa wafungwa waliofungwa kwa makosa madogo madogo, kwani majambazi na wenye makosa mengine makubwa hawatopewa nafasi ya kutolewa.

Pia amesema kuwa baadaye atamtafuta Mh.Rais John Pombe Magufuli ili kuzungumzia juu ya kuwapa dhamana wafungwa wanaostahili kupewa msaada wa parole ili wakatafute pesa kwa ajili ya kulipia faini yao na sio kuzidi kuwajaza wafungwa.

Katika hatua nyingine Mremaa amesema hali ya wafungwa magerezani ni mbaya kutokana na kurundikana magerezani na kuahidi kuwa hadi kufikia krismasi wafungwa walio na sifa ya kupata msaada wa parole watakuwa wameachiwa ili kupunguza msongamano wa wafungwa na mahabusu kwani mahabusu waliopo sasa ni kama 17,000 na wafungwa waliyopo ni kama 15,000.

Amesem anajitahidi pia kuzuia watu wengi kupelekwa gerezani kwa kuangalia maeneo yanayozalisha wafungwa watarajiwa au mahabusu watarajiwa kukaa nao na kuwaambia juu ya hali mbaya iliyopo magerezani ili kupunguza msongamano wa mahabusu na wafugwa. 


Ametolea mfano suala la Ukuta na kusema kuwa endapo maandamano yaliyokuwa yamezuiwa na Rais kufanyika yangefanyika basi kuna watu wangeingia mahabusu au gerezani pasipo kuwepo na ulazima wa kufanya hivyo.

Kuhusu suala la kubambikiwa kesi amekiri kuwepo kwa malalamiko ya watu kubambikiwa kesi na kudai kuwa amejaribu kulifuatilia kwa kukutana na watu wanaolalamika, na moja kati ya aliokutana nao ni madereva boda boda wa wilaya ya kinondoni na kuelezwa juu ya polisi wasio wa serikali kuwakamata kwa makosa yasiyokuwa na uhalali na kusema kuwa polisi hao “polisi jamii” sio halali na wamewekwa na watu fulani, akisema wanatumika visivyo kutokana na mtandao uliopo katika jeshi la polisi.

Amesema kuwa hao polisi hawana mshahara na kuhoji wanalipwa na nani? Amesema Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Tanzania, Naibu Kamishna Mohamed Mpinga alikiri kuwa hao ni waalifu, na hawana sababu ya kutumia neno polisi jamii {polisi shirikishi}, akisema hao ni polisi tu wa kukusanya hela kwa kuwa haijulikani polisi hao wanalipwa mshahara na nani.



Mafanikio yake anayojivunia wakati akiwa Mbunge wa jimbo la Vunjo ukizungumzia wabunge ambao wameshawahi kufanya mambo makubwa katika majimbo yao na yanaonekana hadi leo basi pia utakapomtaja Rais wa sasa wa tanzania Dr. John Pombe Magufuli huwezi kumuacha aliyewahi kuwa mbunge wa jimbo la Vunjo Mh. Augustino Lyatonga Mrema.

Moja kati ya maendeleo anayojivunia hadi sasa ni kusimamia ujenzi wa Barabara ya Marangu Mtoni hadi Kilema Sokoni pia ile ya Kawawa hadi Nduoni Vunjo Mangaribi lakini pia zipo nyingine nyingi ambazo zilikuwa kwenye mikakati ya kukamilika kama mambo yangeenda vizuri.

Uhamasishaji wa ujenzi wa soko la kimataifa la Local Lover ambapo kwa mujibu wa Mh. Mrema ni kwamba maandalizi yalianza vizuri ya ujenzi wa soko hilo licha kuwa kwa sasa hana uhakika linaendeleaje.

Mh. Mrema anasema kuwa iwapo soko hilo lingemalizika lingewafikisha wafanyabiashara wa kimataifa wakiwemo wa Kenya na Uganda ili kuuza nafaka na biashara nyinginezo.

Mh Mrema amezungumzia kwa ufupi juu ya Parole. “parole ni utaratibu wa kisheria unaomuwezesha mfungwa kukamilisha sehemu ya kifungo chake alichopangiwa nje ya gereza, na moja ya masharti ni lazima awe amekaa gerezani kipindi kisichopungua miaka minne au ametumikia theluthi moja ya kifungo chake, lakini pia suala la tabia yake linazingatiwa ambapo lazima iwe imewaridhisha wakuu wa gereza”.

Pia ameyataja makosa ambayo hayana uhusiano na bodi hii kuwa mfungwa au mahabusu asiwe amehukumiwa kifungo cha maisha, ujambazi wa kutumia silaha, ubakaji, mauaji au uuzaji wa madawa ya kulevya.

Ameongeza kuwa endapo mfungwa akikidhi vigezo hivyo ndipo utaratibu utafuatwa ambapo maafisa wa parole watajadiliana kuandika ripoti ya mfungwa ya kujutia makosa itajadiliwa pia na bodi ya parole ya mkoa kisha watakaporidhika ndipo watakuwe kuiwakilisha katika bodi ya parole ya taifa.


Na Denice Kazenzele-Malunde1 blog Dodoma

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527