
Na Bora Mustafa, Arusha.
Kutokana na ongezeko kubwa la uzalishaji wa taka ndani na nje ya hifadhi, Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori Mweka kimeanzisha programu mpya ijulikanayo kama Environmental and Waste Management, ikiwa na lengo la kuimarisha usimamizi wa mazingira na kulinda hifadhi za taifa.
Akizungumza katika maonesho ya wiki ya Siku ya Wanyamapori Duniani yanayoadhimishwa kila Machi 3, jijini Arusha, Afisa Udahili wa Chuo hicho, Vitalis Joel Kabonda, amesema kuwa uzalishaji mkubwa wa taka umesababisha changamoto ya uchakataji usio wa kitaalamu, hali inayoweza kuhatarisha mazingira ya hifadhi pamoja na usalama wa wanyamapori.
Ameeleza kuwa chuo kimebaini umuhimu wa kuwa na programu maalum itakayozalisha wataalamu wenye ujuzi wa kuchakata na kusimamia taka kwa njia sahihi, salama na inayozingatia misingi ya uhifadhi wa mazingira.
Kupitia programu hiyo, wahitimu watawezeshwa kubadili taka kuwa rasilimali, na hivyo kuifanya kuwa fursa ya kiuchumi huku wakihakikisha mazingira yanatunzwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.
pia amewataka wadau wa uhifadhi na jamii kwa ujumla kuunga mkono juhudi hizo ili kuhakikisha hifadhi zinaendelea kuwa salama na endelevu.
Social Plugin