HUU NDIYO UGONJWA UNAOATHIRI ZAIDI WATU WEUSI

TAFITI mbalimbali zilizofanyika ulimwenguni hasa Marekani zinaonesha watu weusi (Waafrika) na wenye asili ya Bara la Asia ndiyo ambao huathirika zaidi na ugonjwa wa Lupus kuliko wazungu

Hayo yameelezwa Dar es Salaam leo Juni mosi na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Figo na Lupus (Rheumatorogist), Francis Furia alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu ugonjwa huo.
Akifafanua, Dk. Furia ambaye pia ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Tiba na Sayansi  Shirikishi Muhimbili (Muhas)  amesema ugonjwa huo huweza pia kuthiriwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kupitia vinasaba.
Amesema wagonjwa wa Lupus huweza kudhaniwa kuwa ni waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi kwani husababisha kinga zao hushuka na huonekana kuwa dhaifu.
“Wapo ambao hupimwa hadi mara saba wakidhaniwa ni waathirika lakini kila wakipimwa wataalamu hawaoni kitu, na baadae hugundulika ni ugonjwa wa Lupus, ” amesema.
Amesema hata hivyo sasa wanagundulika mapema kwani mifumo ya afya ya uchunguzi imeimarishwa kuliko ilipokuwa zamani.
“Wiki hii nimeona wagonjwa watatu wakiwamo wakubwa kwa watoto, huonesha dalili mbalimbali na wengine huonesha kama wana magonjwa ya figo au akili lakini tukiwaona tuna uwezo wa kutambua wanasumbuliwa na lupus na kwa kutumia vipimo vya kina vya uchunguzi, ” amesema.
Aidha Dk. Furia amesema tafiti iliyowahi kufanyika nchini Marekani inaonesha ugonjwa huo ushambulia zaidi wanawake kuliko wanaume na huwapata zaidi watu walio katika umri wa kuzaa.
“Tafiti zinaonesha kati ya watu wanane hadi 15 wenye ugonjwa huo, mwanaume huwa ni mmoja pekee na waliobaki huwa ni wanawake, Aidha, kwa kundi la watoto wenye ugonjwa huo uwiano huwa ni mwanaume mmoja kati ya watu watatu, ” amesema.
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527