WIZARA YA AFYA YAMWAGA AJIRA 8,000 SEKTA YA AFYA NCHINI

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imepata kibali cha Ajira kwa sekta ya afya nchini cha kuwaajiri wataalam wa kada mbalimbali za Afya wapatao 8,000.


Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Mpoki Ulisubisya.


Dkt. Mpoki amesema wamepata kibali hicho kutoka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na kuongeza kwamba Wizara yake inalo jukumu la kuwapangia vituo vya kazi waombaji wenye sifa kwa mujibu wa waraka wa Maendeleo ya Utumishi wa Umma Namba 1 wa mwaka 2009 kuhusu miundo ya utumishi wa kada za afya chini ya Wizara ya Afya.


Aidha, alisema kibali hicho chenye aina mbili za mwajiri ikiwepo nafasi 6,180 ambazo zimeenda Hospitali zilizo katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwenye hospitali za Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati. 


Nafasi 1,820 zimeenda Hospitali zilizo chini ya Wizara ya Afya, Hospitali za Rufaa za Mikoa, Wizara zingine na Taasisi za Umma pamoja na Hospitali ya Mlongazila na Benjamini Mkapa.


Alitaja sifa za waombaji wa nafasi hizo kuwa, awe raia wa Tanzania, umri usiozidi miaka 45, asiwe mwajiri wa Serikali au mwajiriwa wa Hospitali za Mashirika ya Dini ambaye mshahara wake unalipwa na Serikali na asiwe ameshawahi kufanya kazi Serikalini na kuacha kazi.


Hata hivyo, Dkt. Mpoki amewakumbusha wataalam hasa wale wanaosajiliwa na mabaraza ya kitaaluma kuambatanisha nakala za usajili au leseni ya kufanya kazi ya taaluma husika wakati wa maombi hayo.


Katibu Mkuu ameishukuru Serikali ya Awamu ya Tano na kueleza kuwa nafasi hizi 8,000 ni juhudi za Serikali za kupunguza uhaba wa rasilimali watu katika sekta ya afya.


Imetolewa na :
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Afya
11/5/2018

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527