DC SHINYANGA APIGA MARUFUKU UNUNUZI HOLELA WA PAMBA


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro amepiga marufuku ununuaji na uuzaji holela wa pamba na kwamba makampuni na  watu binafsi watakaokiuka maagizo hayo atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Matiro alitoa agizo hilo leo Mei, 2018 kwa wakulima wa kata ya Iselamagazi iliyopo katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga  kwenye mkutano wake wa hadhara juu ya umuhimu wa kujiunga kwenye vyama vya ushirika, kuwa marufuku uuzaji wala ununuzi wa zao la pamba Kiholela, na atakaye bainika kukeuka maagizo hayo atashughulikiwa. 

Alisema serikali imeshatoa maagizo kuwa pamba yote ya mkulima itauzwa kupitia Vyama vya ushirika (AMCOS), ambavyo vimeshaundwa na vile vilivyokuwa vimeshakufa kufufuliwa kwenye vijiji vyao kwa lengo la kuondoa changamoto ya kumyonya mkulima na kumuinua kiuchumi. 

“Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alishapiga marufuku zao la pamba kuuzwa ama kununuliwa kiholela, bali liuzwe kupitia vyama vya ushirika, na sisi watendaji wa serikali tunalitilia mkazo agizo hilo, na ndiyo maana tumeshaunda vyama vya ushirika kila kijiji pamoja na kuvifufua vile ambavyo vilikuwa vimeshakufa,” alisema Matiro. 

“Ni marufuku kampuni, mtu binafsi kununua pamba kwa wakulima na atakaye bainika kwenda kinyume na agizo hilo, serikali itamchukulia hatua kali za kisheria, tunataka mkulima wa zao la pamba ainuke kiuchumi pamoja na kurudisha heshima ya dhahabu nyeupe,”aliongeza Matiro. 

Aidha alitoa wito kwa wakulima kufungua akaunti kwenye taasisi za kifedha (benki) kwani katika msimu wa mwaka huu hakuna mkulima ambaye atalipwa pesa mkononi, bali zitakuwa zikilipwa kupitia akaunti zao, kwa lengo la kulinda usalama wa maisha yao na kuondoa matumizi ambayo siyo ya lazima. 

Naye Ofisa ushirika wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Shija Mwika alisema mpaka sasa kwenye halmashauri hiyo kuna vyama ushirika 45 huku vingine vikiendelea kuundwa, na kutoa msisitizo kwa wakulima kuendelea kujiunga kwa sababu watapata faida nyingi ikiwamo na kupata pembejeo kwa wakati. 

Nao baadhi ya wakulima wa pamba kwenye kata hiyo wameipongeza serikali kwa kupiga marufuku hiyo ya ununuzi wa pamba kiholela, kitendo ambacho kilikuwa kikimyonya mkulima hasa kwenye upunjwaji wa kilo na kumkandamiza kiuchumi.

Imeandikwa na Marco Maduhu - Malunde1 blog & Shinyanga News blog
TAZAMA HABARI PICHA HAPA CHINI 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na wananchi wa kata ya Iselamagazi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga - Picha na Marco Maduhu - Malunde1 blog & Shinyanga News Blog
Wananchi wa Kata ya Isemagazi wakiwa kwenye mkutano wa mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro juu ya umuhimu wa kujiunga na vyama vya Ushirika, pamoja na kuhamashishwa pia kujiunga na mfuko wa bima ya afya ya CHF iliyoboreshwa ili kuwapunguzia gharama za matibabu.
Wananchi wa kata ya Iselamagazi wakiwa kwenye mkutano wa hamasa ya kujiunga na vyama vya ushirika.
Wananchi wa kata ya Iselamagazi wakiwa kwenye mkutano huo
Wananchi wa kata ya Iselamagazi wakimsikiliza mkuu wa wilaya
Wananchi wa kata ya Iselamagazi wakiwa kwenye mkutano huo
Mkutano unaendelea
Mkutano unaendelea

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527