MTENDAJI WA KATA AUAWA KWA KUPIGWA RISASI KISHA KUKATWA MAPANGA


Mtendaji wa Kata ya Mwandui iliyopo mwambao wa bonde la ziwa Rukwa, wilayani Sumbawanga mkoani hapa, Benedict Chapewa ameuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, George Kyando amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo, Mei 2,2018.

Kamanda Kyando amesema Chapewa ambaye amewahi kuwa Katibu Mwenezi, CCM Wilaya ya Sumbawanga, alivamiwa na kundi la watu wasiojulikana wakati akiwa anakunywa pombe katika moja ya baa anayomiliki kijijini hapo.

“Watu hao walimmiminia risasi kwa kutumia bunduki aina ya gobore kisha kumkata kata na mapanga sehemu mbalimbali za mwili wake,” amesema.

Amesema baada ya wauaji kutekeleza adhima yao waliondoka kuelekea kusikojulikana na hawakuchukua kitu chochote kutoka kwa marehemu au katika baa hiyo.

Kamanda Kyando amesema uchunguzi wa kina kuhusu tukio hilo unaendelea kufanyika na watuhumiwa wanasakwa popote walipo ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Ametoa wito kwa wananchi wa mkoa huo kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi kwani kufanya hivyo ni ukiukaji wa haki za binadamu na vyombo vya dola vitahakikisha vinawachukulia hatua za kisheria wale wote wanajichukulia sheria mkononi.

Na Mussa Mwangoka, Mwananchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527