MAKONDA AIBUKA NA KAMPENI YA KUPIMA TEZI DUME NYUMBA KWA NYUMBA


Wakati chanjo ya saratani ya mlango wa kizazi kwa wasichana wote wenye umri wa miaka 14 ikitarajiwa kuanza kutolewa Jumatatu wiki ijayo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amesema ana mikakati ya kupita nyumba kwa nyumba ili kuwapima wanaume saratani tezi ya dume.


Makonda ameyasema hayo leo Aprili 21,2018 wakati akifungua rasmi warsha ya chanjo hiyo iliyowashirikisha waandishi wa habari, wataalamu wa afya, viongozi mbalimbali wa dini na siasa.

Amesema wakati saratani ya mlango wa kizazi ikiwaathiri wanawake nchini, tezi dume inaumiza zaidi akina baba ambao hata hivyo hakuna mwamko wa kulizungumzia jambo hilo katika jamii. 

"Kuna kasumba kuwa saratani ya tezi dume inapimwa kwa kidole jamani siyo kweli, kuna kipimo cha damu na ni rahisi hivyo nina mkakati wa kupita nyumba kwa nyumba katika mkoa wangu kuhakikisha hii kasi ya vifo kwa kinababa inapungua kwa kuwagundua mapema na kuwaanzishia matibabu," amesema Makonda. 

Pia, ametoa wito kwa viongozi wote wa serikali za mitaa na viongozi wa dini kuhakikisha wanatoa elimu kwa jamii ili wasichana wote wenye umri huo wafike kwenye vituo kwa wingi kupata chanjo.

Makonda amesisitiza pia kuzingatia kupata chanjo kamili kwa kurudi mara ya pili ili kuikamilisha. 

Na Herieth Makwetta, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527