AFUKUZWA KAZI AKIFUATILIA PENZI LA DIAMOND NA ZARI


Sakata la kuvunjika kwa penzi la mwanamuziki Diamond Platnumz na Zari The Bosslady halijapoa na sasa limemuondoa mpiga picha wake, Andrew Kisula maarufu Kifesi ambaye ametangaza kuacha kufanya kazi naye baada ya kuwapo tetesi kuwa anaweza kufukuzwa.

Tetesi za uwezekano wa kufukuzwa kwa mpiga picha huyo zilianza kuzagaa jana asubuhi zikihusishwa na kitendo cha kumuandikia waraka mzito bosi wake akimsihi asiachane na Zari kwa kuwa ni mwanamke mwenye akili.

Kupitia mtandao wa Instagram, Kifesi aliandika: Blaza angu Chibu, hivi kweli ndio umekubali huyu mwanamke wa baraka uliopewa na Mungu akakupa na kafamilia kazuri aende. Duh haya bana.. Akili ni nywele kila mtu ana zake.”

Ilielezwa kuwa kauli hiyo haikuufurahisha uongozi wa WCB ambao Diamond anauongoza na kupanga ‘kumshughulikia’ mapema wiki ijayo.

Kuthibitisha kuwa kuondoka kwa Kifesi kunahusiana na tukio la Zari, dada wa mwanamuziki Diamond, Esmah aliandika katika mtandao huo akifafanua kuwa kilichomwondoa ni kuingilia maisha ya bosi wake.

Esmah alikuwa miongoni mwa watu waliotoa maoni katika tamko la mpiga picha huyo la kutangaza kujiondoa katika kazi hiyo akisema aache kusema uongo.

“Acha uongo Kifesi sema umefukuzwa, kuacha kazi kufuatilia maisha ya bosi wako. Yametushinda sie utayaweza mtu baki,” alihoji Esmah ambaye ni mfanyabiashara wa vitenge.

Chanzo- Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527