LUNDENGA ATANGAZA KUACHANA NA MASHINDANO YA MISS TANZANIA

Mkurugenzi wa Kampuni inayoandaa mashindano ya Miss Tanzania ya Lino International Agency LTD Hashim Lundenga ametangaza rasmi kuacha shughuli za kuendesha mashindano hayo kuanzia Februari 13 mwaka huu.


Hivyo kuanzia sasa mashindano ya Miss Tanzania nchini yataendeshwa na The Look Company Limited, chini ya Mkurugenzi Basilla Mwanukuzi aliyewahi kuwa Miss Tanzania mwaka 1998.


Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hashim Lundenga amesema uamuzi huo umetokana na malengo yao ya kutaka mashindino hayo kusimamiwa na damu changa kwa lengo la kuleta chachu katika tasnia ya urembo nchini.


“Tumefikia uamuzi huu baada ya kuona kampuni yetu tayari imejijengea sifa na heshima nchini.Hata hivyo tunaamini The Look Company Limited chini ya Mkurugenzi Mwanukuzi watasimamia taratibu, kanuni, sheria na miiko ya uongozi na hatimaye kumpeleka mrembo katika mashindano ya dunia kama ilivyo kawaida,”amesema. 


Amewataka waandaaji wapya wa mashindano ya urembo wasisite kuomba ushauri au mawazo ya kujenga kutoka kwao pale watakapohitaji.


Lundenga ambaye ni maarufu kama Uncle Hashim amewashukuru Baraza za sanaa la Taifa (BASATA), na Wizara ya Habari, Utamaduni,Sanaa na Michezo kwa ushirikiano mkubwa kwa muda wote tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 1994.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni ya Look Limited, Mwanukuzi amesema wamejiwekea mikakati kuendeleza fani ya ulimbwende pale ambapo kampuni ya Lino imeishia. Amesema kuwa pale penye changamoto katika kuandaa masuala ya warembo watakuwa karibu na Kampuni ya Lino pamoja na BASATA ili kufanikisha na kuleta tija katika Taifa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527