IDADI YA WATANZANIA SASA NI MILIONI 54.2

WAZIRI wa Fedha na Mipango,Dk. Philip Mpango amepiga marufuku kwa shirika lolote kufanya makadirio ya idadi ya watu wa Tanzania na kuchapisha matokeo hayo bila kushirikisha Ofisi ya Taifa ya Takwimu na atakayebainika kufanya hivyo watamchukulia hatua kali za kisheria.


Dk.Mpango amesema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati anazindua taarifa ya makisio ya idadi ya watu Tanzania ambapo alisema kwa makadirio yaliyotokana na Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012.


Viwango vya uzazi na vifo kwa takwimu za mwaka 2016, idadi ya watu Tanzania sasa ni milioni 54.2 ambapo Tanzania Bara ni watu milioni 52.6 na Tanzania Bara watu milioni 1.6 kwa mwaka 2018.


Dk.Mpango alisema idadi hiyo inakadiriwa kufikia watu milioni 59.4 mwaka 2021 na ifikapo mwaka 2030 idadi ya watu itafikia milioni 77.5.


Pia Dk.Mpango aliwakumbusha wadau wote wa ndani na nje ya nchi kuwa takwimu za idadi ya watu kwa nchi ya Tanzania ni hizo ambazo amezitangaza jana na si vinginevyo.


Alifafanua kwa kuzingatia matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 inakadiriwa kuwa kila mwaka kuna ongezeko la wastani watu wapatao milioni 1.6 hapa nchini.


Dk.Mpango alisema ongezeko hill linatokana na idadi kubwa vya vizazi vipatavyo milioni 2.0 ikilinganishwa na idadi ndogo ya vifo ambavyo ni takribani 400,000 kwa mwaka.


“Utafiti wa mama na mtoto wa mwaka 2015/16 unaonesha kwamba mwanamke wa kitanzania atazaa watoto watano katika maisha yake yote ya uzazi .


” Hata hivyo kiwango cha uzazi kilipungua kutoka wastani wa watoto 7 mwaka 1978 had I wastani wa watoto watano mwaka 2016.Baadhi ya sababu za juu cha uzazi ni kiwango kikubwa cha vifo vya watoto,familia kupendelea kuwa na watoto wengi,umasikini,mila,imani za kidini na matumizi madogo ya uzazi wa Mpango,”alisema.


Aliongeza matokeo yake ni kuwa na idadi ya watu hapa nchini imeendelea kuongezeka na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya sita katika Bara la Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya watu baada ya Nigeria, Ethiopia, DRC na Misri.


Alisema kwa mtazamo wake wingi au au uchache wa idadi ya watu sio tatizo bali tatizo ni pale ambapo kasi ya ongezeko la idadi hiyo inazidi kasi ya ukuaji wa uchumi na hivyo kulifanya Taifa kushindwa kumudu ipasavyo mahitaji ya wananchi.


Dk.Mpango alisema kasi ya ongezeko la idadi ya watu pia inaleta changamoto ya idadi kubwa ya watoto na vijana .”Kwa mfano takwimu nilizozizindua leo zinaonesha asilimia 50 ya watu wote nchini ni watoto wenye umri chini ya miaka 18.


“Asilimia hii kubwa ya watoto katika nchi zinazoendelea inatokana na mabadiliko ya kidemografia kutoka viwango vya juu vya vifo lakini wakati huo viwango vya uzazi vibaki juu,” alisema.


Aliongeza asilimia kubwa ya watoto ni changamoto kwa maendeleo ya nchi yoyote duniani kwa vile kundi hilo lina mahitaji ya kipekee ambayo lazima yatimizwe na Serikali na jamii kwa ujumla wake.


Dk.Mpango alisema mojawapo ya changamoto hizo ni kiwango cha juu cha utegemezi kinachotokana na idadi kubwa ya watoto.


Alisema kwa mfano kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 kiwango cha utegemezi kiumri ni asilimia 92 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 40 kwa nchi zinazoendelea.


Hiyo ikiwa na maana kuwa kwa Tanzania kila watu 100 wenye umri wa miaka 15 hadi 64 wanategemewa na watu 92 wenye umri chini ya miaka 15 wenye umri zaidi ya miaka 65.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527