AFANDE SELE AJIUNGA CCM MBELE YA JPM

Msanii mkongwe nchini Afande sele ametangaza rasmi kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM) leo mbele ya Rais Dkt. Magufuli kwa lengo ka kuunga mkono jitihada zake anazozifanya katika kupigania na kukiomba chama kimpokee kama kijana wao



Afande Sele ametoa kauli hiyo wakati alipokuwa anatumbuiza muziki kwa wananchi wa mkoa wa Morogoro walioweza kuhudhuria shughuli za uzinduzi wa kiwanda cha Sigara mkoani humo na Rais Magufuli.


"Nataka nimuhakikishie Mhe. Rais Dkt. John Magufuli kwamba mimi ni mtu wakufikiri, mbishi na mgumu sana katika kukubali jambo fulani lakini niseme kwa uwazi kabisa tangu ulipochukua madaraka ya kuwa Rais na Mwenyekiti wa CCM umeweza kuinyosha nchi na kukisafisha chama chako na kimeweza kurudi katika uimara wake kama alivyokuwa anataka muasisi wetu wa taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere lakini leo kimekuwa hivyo", amesema Afande Sele.


Pamoja na hayo, Afande sele ameendelea kwa kusema "naomba nikupongeze sana kwa hilo lakini kama haitoshi naomba nikuhakikishie kwamba leo hii kutoka kwa dhati ya moyo wangu nimeamua nisimame upande mmoja na wewe ili nisiachwe katika maendeleo. 


"Ninaamini kabisa Mhe. Rais sasa hivi Tanzania kama gari basi dereva ametulia na gari linakwenda na mimi kama abiria niachwe ninywe soda yangu kwa amani kwasababu naamini kabisa chombo chetu kinaenda sehemu salama na sipendi kesho historia ije kunihukumu kwa watu wale ambao hawakuchangia walichonacho katika kufikisha mahali kinapoenda.


"Nawaomba viongozi ngazi ya mkoa wa CCM mnipokee kijana wenu nije kuongeza nguvu", amesisitiza Afande sele.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527