POLISI YADAI MAUAJI YA DIWANI WA CHADEMA NI YA KULIPIZA KISASI

Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro limesema mauaji ya diwani wa kata ya Namwawala kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Godfrey Luena huenda yametokana na ulipizaji kisasi wa mauaji ya mwaka 2016.


Luena aliuawa juzi usiku baada ya kuvamiwa na watu wasiojulikana nyumbani kwake wilayani Kilombero.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei alisema jana kuwa watu wasiojulikana walizima umeme nyumbani kwake na kumvamia kwa mapanga na kwamba baada ya mauaji hayo hawakuchukua kitu chochote.


“Marehemu amejenga pembezoni kidogo ya msitu," alisema Kamanda Matei. "Baada ya mauaji watu hao walikimbilia msituni".


"Polisi wanaendelea na uchunguzi zaidi na kiini cha tukio hili Jeshi la Polisi linasema ni kisasi. Baada ya wauaji hawakuchukua kitu chochote.”


Kamanda Matei alisema taarifa za awali zinahusisha kifo hicho na kile cha mkazi mwingine wa Namwawala, Keenan Haule, kilichohusishwa na ushahidi na mgogoro wa mashamba ambao kesi yake inaendelea Mahakama Kuu.


“Mwanzoni mwa mwaka 2016 wananchi wa Namwawala walikuwa na ugomvi na Bodi ya Sukari kuhusiana na mashamba," alisema Kamanda Matei, na "marehemu akiwa diwani wa eneo lile alisimamia kudai mashamba hayo.


"Kuna kesi iko Mahakama Kuu inaendelea hadi sasa."


Kamanda Matei alisema wakati huo marehemu Luena aliwaambia wananchi kuwa marehemu Haule ambaye aliuawa 2016 ndiye msaliti wao na kwamba kama angefariki wangeweza kupata mashamba wanayogombea.


"Muda mfupi baadaye Kenan (Haule) aliuawa kwa kukatwa na mapanga tukio ambalo lilitokea kama ilivyotokea kwa marehemu Luena.”


Kamanda Matei alisema uchunguzi wa shauri hilo alilodai ni baya kutokea kwa mkoa wa Morogoro bado unaendelea sambamba na kuwasaka watuhumiwa wa tukio hilo.


Alitoa wito kwa watu wanaofahamu taarifa kuhusiana na mauaji hayo kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola ili waweze kuchunguza na kuchukua hatua mara moja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527