MGOMBEA WA CHADEMA ATOWEKA KWENYE MAZINGIRA YA KUTATANISHA

WAKATI kampeni za ubunge na udiwani zikiendelea, mgombea udiwani (Chadema) Kata ya Buhangaza wilayani Muleba amepotea katika mazingira ya kutatanisha.

Imeelezwa alipotea Februari 2,2018 alipokuwa akitokea Bukoba mjini kwenda nyumbani kwake Kijiji cha Buhangaza ikidaiwa ametekwa.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Isack Msangi amethibitisha kupokea taarifa za kupotea kwa mgombea huyo.

Amesema kuwa hawana madai kuwa ametekwa bali aliondoka nyumbani na hajarejea.

Msangi amesema polisi inawaomba wananchi kutoa ushirikiano bila kupotosha au kuegemea upande mmoja wa kisiasa kwa kutuhumu upande mwingine bali waungane kufanikisha kupatikana kwake.

Katibu wa uenezi wa Chadema jimbo la Muleba Kusini na mratibu wa chama hicho jimbo la Muleba Kaskazini, Hamisi Yusufu alisema jana Februari 4,2018 kuwa mgombea huyo ni Athanasio Makoti (28).

Yusufu alisema Makoti ambaye ni Mchungaji wa Kanisa la AGT anashiriki uchaguzi mdogo wa udiwani utakaofanyika Februari 17. Anachuana na mgombea wa CCM, Jenitha Tibeyenda na wa NCCR -Mageuzi, Grason Anaseti.

Alisema Februari 2,2018 saa 12:00 jioni akitumia simu yake ya mkononi aliwajulisha viongozi wa Chadema ngazi ya wilaya kuwa alipanda gari lenye watu wanne kutoka Kijiji cha Mafumbo njia panda ya kwenda Kamachumu akielekea Kijiji cha Buhangaza.

Yusufu alisema baadaye ujumbe mfupi wa maneno (sms) ulitumwa kwa Advera Kalikwela, diwani wa viti maalumu (Chadema) Kata ya Ijumbi ukieleza, “Nimeteremka hapa Mafumbo kabla ya kufuatwa na bodaboda wangu nimezingirwa na gari lenye watu wanne mmoja mwanamke, mbele dereva wa kiume na vijana wengine wawili ni kama nimetekwa.”

Alisema baada ya ujumbe huo, simu ya Makoti iliita bila kupokewa na hadi sasa hakuna taarifa za kuonekana kwake na kwamba familia ilitoa taarifa polisi.

Egbert Makoti ambaye ni mdogo wa mgombea huyo amesema baada ya kuchukua fomu, ndugu yake aliwaeleza kuna watu ambao hakuwataja waliomtaka aachane na kata hiyo wakimtaka apokee Sh8 milioni lakini alikataa.

Katibu wa Baraza la Wazee la Chadema, Rodrick Lutembeka amesema chama hicho kitaendelea kumnadi katika kampeni zinazoendelea katika Kata ya Buhangaza.

Kata hiyo ina vijiji vitatu vya Buhangaza, Kashenge na Buyaga ikiwa na vitongoji 13 ikikadiriwa kuwa na zaidi ya wapiga kura waliojiandikisha 2,500.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527