WAZIRI MKUU AUVUNJA MFUKO WA WAKFU WA KUENDELEZA ZAO LA KAHAWA - CDTF

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameuvunja Mfuko wa Wakfu wa Kuendeleza zao la Kahawa (CDTF) na amemuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuchunguza mwenendo wa mfuko huo tangu ulipoanzishwa.


Ametoa agizo hilo jana (Jumapili, Januari 14, 2018) wakati akizungumza na wadau wa zao hilo kwenye kikao cha kujadili maendeleo ya zao la kahawa alichokiitisha, mjini Dodoma.


Waziri Mkuu amechukua hatua hiyo baada ya kubaini kwamba uundwaji wa mfuko huo si wa kisheria bali ni wadau wa zao hilo kwa kushirikiana na Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB).


“Wakati Serikali inapambana kupunguza makato ya hovyo kwa wakulima, kumbe huku kuna chombo cha kuwachukulia fedha wakulima hii haikubaliki.”


Pia aliagiza kufungwa kwa ofisi za CDTF ili kupisha uchunguzi na baada ya CAG kukamilisha uchunguzi na kukabidhi ripoti, kazi zote zilizokuwa zinafanywa na mfuko huo zitafanywa na Bodi ya Kahawa.


Hata hivyo, Waziri Mkuu ameongeza kuwa majukumu ya kuundwa kwa mfuko huo yanaingiliana na yale ya Bodi ya Kahawa, ambayo ni pamoja na kufuatilia maendeleo ya zao hilo, hivyo hakuna haja ya kuwa vyombo viwili vinavyofanya kazi moja.


Wakati huo huo, Waziri Mkuu amepiga marufuku wanunuzi wa kahawa kwenda kununua kwa wanavijiji na badala yake kahawa yote itauzwa kwa njia ya minada.


“Kahawa itauzwa katika minada tu na utaratibu wa kutoa vibali kwa wanunuzi wa kahawa kwenda kununua kwa wananchi vijijini marufuku kuanzia sasa, kama kuna watu wamepeleka fedha zao wazirudishe kwani hazitafanya kazi.”


Amesema Wakuu wa Mikoa na Wilaya wasimamie uuzwaji wa zao hilo na kuwachukulia hatua wote watakaokutwa wananunua kahawa kwa wakulima. “Anayetaka kahawa akanunue mnadani na si kwa wanavijiji lengo ni kuhakikisha mkulima anapata tija.”


Pia ameziagiza halmashauri zote zinazolima kahawa nchini kuanzisha vitalu vya miche ya kahawa na kisha kuigawa bure kwa wakulima, pia Maofiza Kilimo wawaelimishe walkulima wote wenye miti mikongwe waanzisha mashamba mapya.


Kuhusu suala la utafiti wa zao hilo, Waziri Mkuu ameiagiza Wizara ya Kilimo itumie vyuo vyake vya kilimo ianzishe vituo vyake vya utafiti vitakavyofanya kazi ya utafiti wa zao hilo.


Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Bw. Joseph Kakunda amesema watahakikisha maagizo hayo yanafanyiwa kazi, ambapo aliwaagiza Wakuu wa mikoa yote 16 inayolima kahawa pamoja na wakuu wa wilaya wake 52 wahakikishe wanafuta mara moja vibali vya ununuzi wa kahawa katika vyanzo vyao vya mapato.


Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina mjini Dodoma kilihudhuliwa na Waziri wa Kilimo Dkt. Chales Tizeba, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Bw. Charles Mwijage, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Bw. Kakunda.


Wengine ni Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu,, Bibi Maimuna Tarishi, Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Mhandisi Mathew Mtigumwe, Wakuu wa mikoa 16 wanaolima kahawa na wakuu wa wilaya,Mrajis wa Vyama vya Ushirika Nchini, Dkt. Tito Haule, Makatibu tawala wa mikoa inayolima kahawa.


Mwenyekiti wa Bodi ya Kahawa na wajumbe wa bodi hiyo,,Mkurugenzi wa bodi ya Kahawa Tanzania, Wakurugenzi wa Halmashauri,


IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527