TANZANIA YAIBUKA KINARA AFRIKA UCHUMI JUMUISHI

Baada ya Tanzania kuibuka kinara wa Uchumi Jumuishi barani Afrika, baadhi ya Wataalamu wa masuala ya uchumi nchini wameelezea kuwa hatua zinazochikuliwa na Serikali kuwawezesha wanachi kuwekeza katika shughuli za kiuchumi na utoaji bora wa huduma za jamii vitaufanya uchumi wa Tanzania kuendelea kukua zaidi.



Wakitoa maoni yao juu ya dhana ya uchumi jumuishi, baadhi ya wataalamu hao wamesema kuwa madiliko ya sera na sheria zinawawezesha wananchi wengi kumiliki uchumi ni sehemu ya vigezo vya kuufanya uchumi kukua huku ukigusa maisha ya wananchi walio wengi.


Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi, Bi. Bengi Issa ameielezea dhana ya uchumi jumuishi kuwa ni ile ambayo shughuli za kiuchumi zinawajumuisha moja kwa moja wananchi na kwamba mabadiliko ya sheria katika sekta ya madini na katika umiliki wa makampuni ya simu yametoa fursa kwa watanzania wengi kushirikikatika uchumi.


Amesema kuwa utekelezaji wa sera ya elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi kidato cha nne, kuimarishwa kwa huduma za afya, maji, umeme pamoja na mapambano dhidi ya rushwa, hifadhi ya jamii na utekelezaji wa miradi ambayo inawapa fursa wananchi kushirikikatika shughli a kiuchumi ni miongoni mwa sifa zinazoifanya Tanzania kushika nafasi ya juu.


“Serikali inaweka mazingira bora ya wananchi kushiriki shughuli za kiuchumi katika miradi mbalimbali. Tunahakikisha kila mradi unaoingia nchini basi wafanyabiashara wa Tanzania wanashiriki kikamilifu katika utekelezaji wa mradi huo”, alifafanua Bi. Bengi.


Amesema kwa upande wa Baraza la Taifa la Uwezeshaji Kiuchumi wamekuwa wakishiriki katika kuweka mipango na sera ili kuhakikisha Watanzania wengi wanashiriki shughuli zakiuchumi ikiwemo kumiliki ardhi ili iwasaidie katika kutafuta mitaji ya biashara.


Nae Mtaalam wa Uchumi wa Kilimo ambaye pia aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya ESRF, Dkt. Hoseana Lunogelo anaeleza kuwa mfumo bora wa utawala nchini umewezesha Tanzania kuwa na Uchumi Jumuishi kutokana na wananchi kuanzia ngazi ya kijiji kushirikishwa katika kupanga mipango ya maendeleo jambo ambalo linawafanya waangalie vipaumbele muhimu katika maeneo yao.


Dkt. Lunogelo anataja mradi ya TASAF, kuongezeka kwa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, kuanzishwa kwa vikundi vya kuweka na kukopa (SACCOS) na kurahisishwa kwa huduma za kifedha ni miongoni mwa mambo yanaifanya Tanzania kuibuka kinara katika uchumi jumuishi.


Aidha, Dkt. Lunogelo anaeleza kuwa kutokana na kuendelea kuboreshwa kwa mifumo na juhudi za makusudi za Serikali za kuwasaidia Watanzania wengi zaidi kushiriki shughuli za kiuchumi kutaifanya Tanzania kung’ara zaidi katika suala la uchumi jumuishi ambao unafaidisha wananchi wengi.


“Uchumi jumuishi ndio msingi mkubwa wa kuleta amani na utulivu katika nchi kwani watu wanaguswa na matunda ya ukuaji wa uchumi”, alieleza Mtaalamu huyo wa Uchumi.


Dkt. Lunogelo anasisitiza kuendelea kufanya kuwashirikisha na kuwatafutia wananchi fursa zaidi za kiuchumi ili dhana hii ya Uchumi Jumuishi iwaguse Watanzania wengi zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527