RC SHINYANGA ATUMBUA VIONGOZI WOTE WA KIJIJI KWA KUGEUZA MADARASA KUWA MIGODI YA ALMASI


Mkuu wa Mkoa Mhe. Zainab Telack akiwa na mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu ,Stephen Magoiga wakiangalia uharibifu uliofanywa kwenye vyumba vya madarasa vinavyojengwa baada ya kuchimbwa ili kutafuta madini ya almasi kulikofanywa na wajumbe wa kamati ya shule ya msingi jitegemee kwa kushirikiana na Serikali ya kijiji cha Maganzo wilayani Kishapu.
Sehemu ya darasa iliyoharibiwa kwa kuchimba madini ya almasi katika shule ya msingi Jitegemee, kata ya Maganzo wilayani Kishapu.
Sehemu ya darasa iliyoharibiwa kwa kuchimba madini ya almasi katika shule ya msingi Jitegemee
***
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Zainab Telack ameivunja serikali ya kijiji cha Maganzo na kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu kukagua mapato yote na matumizi ya kijiji hicho ikiwemo fedha zilizochangwa na kutumika kujenga choo na madarasa yaliyochimbwa almasi pamoja na uharibifu uliojitokeza.

Mhe. Telack amefikia uamuzi huo jana Januari 10,2018 wakati wa ziara yake wilayani Kishapu, kufuatia kitendo cha wajumbe wa Kamati ya shule ya msingi Jitegemee pamoja na serikali ya kijiji kuchimba madini kwenye vyumba vya madarasa yanayojengwa kwa lengo la kutafuta almasi.

“Kwa utaratibu mimi ndiye mwenye mamlaka ya kuvunja Serikali ya kijiji na kuanzia leo nimesema Serikali ya kijiji hicho naivunja, tutafanya taratibu za kuchagua Serikali nyingine”,alisema Mhe. Telack.

Alisema wote waliohusika wawajibike kulipa hasara hiyo kwani siyo hasara ya Serikali. Wajaze vifusi na waweke mawe ndani ya madarasa hayo kadri ya maelekezo ya wahandisi wakati taratibu za mahakama zikiendelea.

Viongozi wa kijiji cha Maganzo wanatuhumiwa kuhusika kuchimba ndani ya vyumba vya madarasa yanayojengwa kwa nguvu za wananchi katika shule ya msingi Jitegemee kwa madai ya kutafuta madini ya Almasi pamoja na tuhuma nyinginezo ikiwemo kumkashifu Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Mhe. Nyabaganga Taraba kuwa hafai kuongoza Wilaya hiyo.

Wakati huo huo, Mhe. Telack aliwataka matajiri wanaowatuma vijana maarufu kwa jina la “Wabeshi” wanaoingia kwenye migodi kwenda kuiba mchanga wa almasi uliokwisha chimbwa kuacha mara moja tabia hiyo kwani Serikali haitawavumilia na haitawaacha imejipanga kuwakamata wote.

“Mkawaambie, wakati wao umekwisha, hatutawavumilia na hatutawaacha nadhani mshaona kazi tunayofanya kwa sasa, tuna kikosi maalumu kwa ajili ya kudhibiti wabeshi. Tutawakamata kila mmoja na kuhakikisha Maganzo ni sehemu salama ya kuishi siyo hatarishi”,alisema Telack.

Alisema watu wote wanaotumia fedha zao kuleta uvunjifu wa amani wajue biashara hiyo imeisha kwani watapambana na Serikali, watafute shughuli nyingine za kufanya na watafute mali halali siyo kwa mtindo huo.

Alimtaka Mkuu wa kituo cha polisi wilaya ya Kishapu awakamate wahalifu wote Maganzo wakiwemo viongozi wanaoongoza kwa uvunjifu wa amani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527