HII HAPA GHARAMA YA PASIPOTI YA KIELEKTRONIKI...RAIS MAGUFULI AITAKA UHAMIAJI KUTOOGOPA MTU


 Rais  John Magufuli ameitaka Idara ya Uhamiaji kuhakikisha inapambana na wahamiaji haramu pasipo kumwogopa mtu.

Rais Magufuli  amesema hayo leo Jumatano Januari 31,2018 wakati wa uzinduzi wa hati ya kusafiria ya kielektroniki jijini Dar es Salaam.

Amemwagiza Kamishna wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala kuwachukulia hatua kali watumishi wake watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo.

Amesema utambuzi wa wananchi wanaoishi bila vibali na wenye vibali vilivyoisha ni muhimu na kwamba uhamiaji ina jukumu kubwa katika kutekeleza hayo.

"Haiwezekani wahamiaji haramu wanakamatwa Mbeya halafu wamepita Kilimanjaro, Manyara. Kamishna (Dk Makakala) ifike mahali unapoona hili washushe vyeo, mwondoe nyota moja ili wajue wajibu wao," ameagiza Rais Magufuli.

Amesema awali Uhamiaji iligubikwa na matatizo yakiwamo ya utoaji hovyo wa vibali vya uraia, hata kwa watu ambao walikuwa hawana sifa.

"Kuna raia wengi walipata uraia bila sifa na wapo waliopata uraia na vyeo vya juu kabisa serikalini wakati si raia," amesema.

Dk Magufuli amesema hiyo ndiyo sababu iliyofanya akamteua Dk Makakala kuwa Kamishna. "Wanawake ni waaminifu sana na ameanza kutatua matatizo haya."

Amesema kiasi hicho ni sawa na Sh15,000 kwa mwaka kwa sababu itatumika kwa miaka 10.

Gharama za kupata pasipoti sasa ni Sh50,000 na hutumika kwa miaka 10 tangu zilipotolewa.

Dk Nchemba amesema pasipoti hizo zitakuwa na kurasa nyingi zaidi na mwonekano mpya.

Kamishna wa Uhamiaji, Dk Anna Makakala amesema kuanzia sasa mtu atakayetaka hati ya kusafiria atapaswa kuwa na kitambulisho cha Taifa.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Mwigulu Nchemba amesema gharama ya hati ya kusafiria mpya ya kielektroniki itakuwa Sh150,000.

Amesema hati za sasa zitaendelea kutumika hadi Januari 2020.

Baadhi ya viongozi waliohudhuria uzinduzi huo ni Rais wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein; Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan; na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Wengine ni marais wastaafu Amani Abeid Karume na Ali Hassan Mwinyi; Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma; na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Ali Iddi.

Pia, viongozi wa Serikali, Bunge, Baraza la Wawakilishi, wa dini, wanasiasa, na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527