SERIKALI YA TANZANIA KUANZA KUTOA DAWA ZA KUJIKINGA NA MAAMBUKIZI YA VIRUSI VYA UKIMWI



SERIKALI inatarajia mwakani, kuanza kutoa dawa za kujikinga na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU), ikiwa ni mkakati za kuwazuia watu kutopata maradhi hayo.

Dawa hiyo ni Truvada na utaratibu huo utakuwa wa majaribio na utahusisha watu 12,000 wanaojidunga dawa za kulevya, machangudoa na wanaofanya mapenzi ya jinsia moja. Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Faustine Ndugulile alisema: “Hii ni tiba kama kinga na tutawapima kwanza wote 12,000 na wale wasiokuwa na maambukizi ya VVU ndiyo tutawapa dawa ambao tunajua wanaendelea na ngono zembe, kisha tutafuatilia mienendo yao kwa mwaka mmoja na ikibidi kuongeza iwe miaka miwili.”

Watu hao watakaofanyiwa utafiti huo wa majaribio ni kutoka mikoa ya Njombe, Kagera, Iringa, Mwanza, Mbeya na Dar es Salaam. Dk Ndugulile alisema kutakuwa na timu ya wataalamu ya kufuatilia mienendo yao na afya zao wote watakaokuwa kwenye majaribio hayo. Alisema timu hizo zitagawanywa katika kanda tatu ikiwemo Kanda ya Ziwa.

Alisema dawa hizo watakuwa wakipewa kila mwezi. Vidonge hivyo serikali haijanunua, bali imepata taasisi za Presidents Emergency Plan for Aids Relief (PEPFAR) na Global Fund. “Hizi dawa ni katika mkakati wa kidunia wa kuzuia maambukizi mapya na sisi tumepewa na taasisi hiyo ya Marekani ya PEPFAR na Global Fund,” alieleza Dk Ndugulile.

Dk Ndugulile alisema wanakamilisha taratibu za kuanza kwa majaribio hayo ikiwemo kupata vibali, hivyo hawajajua rasmi lini wataanza kazi hiyo isipokuwa itakuwa mwakani. Sasa hivi nchi nyingi zinatumia Truvada kama kinga dhidi ya maambukizi mapya ya Virusi Vya Ukimwi na miongoni mwao ni pamoja na Kenya, Uganda, Peru na Marekani.

Kwa mujibu wa mtandao wa Truvada.com, utumiaji wa dawa hizo ambao umeidhinishwa na Shirika la Afya Duniani(WHO) una mafanikio makubwa, unaweza kuleta madhara kama ya matatizo ya figo, kuwepo asidi ya lactic nyingi, maumivu ya tumbo, maumivu ya misuli.

Athari nyingine ni kuhema kwa kasi au kasi ya kuhema kuwa chini, kutapika, mapigo ya moyo kuwa katika hali isiyo ya kawaida, tatizo la ini, kichwa kuuma na kupungua uzito. Dawa hiyo ya Truvada imeingizwa nchini mwaka 2013 na imekuwa ikitumika kwenye tiba kama sehemu ya dawa za kufubaza Virusi Vya Ukimwi (ARVs). Inakadiriwa watu milioni 1.4 wanaishi na VVU nchini na maambukizi mapya yameonekana kupungua kila mwaka.

Takwimu zilizotolewa na Tume ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS) zinaonesha mwaka 2013 maambukizi hayo mapya yalikuwa kwa watu 72,000, mwaka uliofuata yalikuwa watu 69,603 na mwaka 2015 yameshuka na kuwa watu 48,000. Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Tacaids, Dk Jerome Kamwela amesema katika semina ya wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ukimwi kadiri dawa za kufubaza virusi vya Ukimwi (ARVs) zinavyoongezeka, vifo vitokanavyo na Ukimwi vinapungua.

Alisema hali ya maambukizi kwa Tanzania ni asilimia 5.3 huku Manyara na Tanga kwa Tanzania Bara, kiwango cha maambukizi kikiwa chini zaidi na Zanzibar, Pemba kipo chini. Makundi yaliyo hatarini zaidi kwa maambukizi na asilimia yao kwa wastani wa kitaifa yakiwa kwenye mabano ni makahaba (26), wanaume wanaofanya mapenzi ya jinsia moja (22.2) na wanaojidunga dawa za kulevya (15). Mengine yaliyo hatarini ni madereva wa malori ya masafa marefu, wafungwa na wafanyakazi wanaohama kufuata ajira

IMEANDIKWA NA ISDORY KITUNDA - HABARILEO

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527