MWANAFUNZI WA CHUO AFARIKI DUNIA MLIMANI AKIFANYA UTALII MOROGORO

Milima ya Morogoro
***
MWANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Kiislamu Morogoro (MUM), Victor Ibrahim (22), amefariki dunia wakati akitalii kwenye milima baada ya kuteleza na kuangukia kwenye korongo.


Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonce Rwegasira, alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea Oktoba 3, mwaka huu, majira ya jioni, katika eneo lenye milima ambalo liko Kata ya Milimani mkoani humo.

Alisema mwanafunzi huyo akiwa na wenzake kwenye hiyo milima, walikuwa wanafanya utalii wa ndani na ndipo alipokanyaga eneo lenye unyevu lililoko kando ya korongo hilo refu na kuangukia kwenye mawe.

Kamanda Rwegasira alisema juhudi za kuutoa mwili wa kijana huyo zilifanikishwa kwa ushirikiano baina ya kikosi cha zimamoto na polisi.

Alisema baada ya uchunguzi kufanyika, polisi waliukabidhi mwili huo kwa familia kwa ajili ya kuendelea na taratibu za mazishi.

Aidha, Kamanda alitoa wito kwa wananchi kuwa wanapotaka kutembelea maeneo kama hayo wahakikishe wanakuwa na watu wa kuwaongoza kwa kuwa wanafahamu sehemu hiyo ili waonyeshwe njia ambazo ni salama.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments